The House of Favourite Newspapers

Aussems Ampa Majukumu Matatu Kocha Simba

0

ALIYEKUWA Kocha Mkuu wa Simba, Mbelgiji, Patrick Aussems, ametamka kuwa kocha ajaye ndani ya kikosi hicho, anatakiwa anatakiwa akifanyie mambo makubwa matatu kama anataka kubaki.

 

Kauli hiyo aliitoa ikiwa ni siku moja baada ya kusitishiwa rasmi mkataba wake wa kuendelea kukinoa kikosi hicho kinachoongoza kwenye msimamo wa Ligi Kuu Bara kikiwa na pointi 25 kikifuatiwa na Kagera Sugar yenye 24, lakini ikiwa na michezo mitatu zaidi.

 

Akizungumza na Championi Jumatatu, Aussems alisema kabla ya kuondolewa Simba alikuwa ana malengo matatu ya kuifanyia timu hiyo kwenye msimu huu wa ligi, kati ya hayo ni kuendelea kuwapa makombe, matokeo mazuri ya ushindi na soka safi la kuvutia.

 

Aussems alisema kuwa anaamini kocha ajaye atafanya hayo mazuri aliyokuwa amepanga kuyatimiza katika msimu huu na hilo linawezekana kutokana na ubora wa kikosi hicho.

 

Aliongeza kuwa anawatakia kila la heri benchi jipya la ufundi, wachezaji, viongozi na mashabiki waliokuwa wanamsapoti katika kipindi chote alichokuwepo akiifundisha Simba na kufanikiwa kutwaa ubingwa wa ligi msimu uliopita na Ngao ya Jamii pamoja na kufika robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

 

“Kwanza niwashukuru mashabiki wote wa Simba waliokuwa wakitumia ujumbe mbalimbali kwa kupitia mitandao ya kijamii wote wakinipa pole na wengine wakinitakia maisha mema nitakapokwenda.

 

“Niwathibitishie mashabiki wa Simba kuwa rasmi hivi sasa siyo kocha wa Simba, ni baada ya kupata taarifa kutoka Bodi ya Wakurugenzi wa Klabu ya Simba, ninaondoka nikiwa bado nina shauku ya kuendelea kuwapa mashabiki furaha kwa kucheza soka la kuvutia, matokeo mazuri ya ushindi na makombe.

 

“Ni matarajio yangu kuona kocha mpya anayekuja Simba anayafanya hayo niliyopanga kuyafanya mimi na hilo linawezekana kutokana na ubora wa timu iliyopo,” alisema Aussems.

Leave A Reply