The House of Favourite Newspapers

Banda ashushiwa rungu Simba

0

Banda 2Kiungo wa Simba, Abdi Banda.

Waandishi Wetu, Dar es Salaam
WAKATI zikiwa zimesalia siku chache kabla ya kurejea kundini beki wa Simba, Hassan Isihaka, upande wa pili, beki mwingine wa timu hiyo, Abdi Banda, ameenguliwa kwenye kikosi hicho kwa sasa kwa kile kilichoelezwa kuwa ni utovu wa nidhamu.

Banda ameripotiwa kuvurugana na kocha wake, Mganda, Jackson Mayanja, kwa kukataa kuingia kuchukua nafasi ya Mohammed Hussein ‘Tshabalala’ kwenye mechi yao ya wikiendi iliyopita dhidi ya Coastal Union ya Tanga.

Mayanja amezungumza na Championi Jumatano juu ya sakata  hilo na kuweka wazi kutofurahishwa na kitendo cha mchezaji huyo na kwamba tayari amemuweka kando katika kikosi chake kitakachoendelea na mazoezi leo kwa ajili ya maandalizi ya mechi zinazokuja.

Aidha, ameeleza kuwa suala la adhabu au kusimamishwa kazi kwa mchezaji huyo halipo tena mikononi mwake bali lipo kwenye himaya ya uongozi ambao watalitolea ufafanuzi na kueleza hatua walizochukua.
“Hakikuwa kitu kizuri kwa Banda kugoma kuingia kucheza, yeye amesaini mkataba kuitumikia Simba, sasa inakuwa siyo sawa kama anapingana na mkataba wake pale anapopangiwa kuitumikia timu halafu anakataa. Nilimtaka aanze kupasha kwa ajili ya kuingia uwanjani lakini badala yake akagoma.

“Sasa vitendo kama hivi siwezi kuviunga mkono hata kidogo ukizingatia amekifanya mbele ya wenzake, itajenga picha mbaya kwa maana na wengine wataiga wakichukulia kuwa ni ishu ya kawaida tu, ndiyo nimeamua kumchukulia hatua na kwa kuanzia hatakuwepo mazoezini wakati inasubiriwa kauli ya uongozi,” alisema Mayanja.

Gazeti hili lilimtafuta Banda ambaye ni mchezaji wa zamani wa Coastal kulitolea ufafanuzi kwa upande wake suala hilo ambapo alisema:

“Kilichotokea ni kwamba Tshabalala alikosea kupiga krosi, kocha akaniambia nipashe nichukue nafasi ya Tshabalala, mimi nikamwambia muache kidogo aendelee kwa sababu kukosea ni kitu cha kawaida lakini ndiyo mwisho nikaona imekuwa ishu kubwa.”

Alipotafutwa Ofisa Habari wa Simba, Haji Manara kuzungumzia ishu hiyo katika ngazi ya uongozi naye alisema kwa kifupi: “Hilo suala tutalizungumzia kesho (leo), tutaitisha kikao maalum kuongea na waandishi wa habari kuhusiana na kila kitu kinachohusu ishu hiyo.”

Hii si mara ya kwanza kutokea kwa kesi kama hiyo chini ya uongozi wa Mayanja baada ya hivi karibuni, Isihaka naye kusimamishwa kwa siku 30 pamoja na kuvuliwa unahodha baada ya kumjibu ‘shombo’ kocha wake huyo katika mchezo wa Kombe la FA dhidi ya Singida United uliopigwa Februari 28, mwaka huu.

Hans Mloli, Said Ally na Sweetbert Lukonge

Leave A Reply