The House of Favourite Newspapers

Chanzo hasa cha upungufu wa nguvu za kiume-3

0

Couple sitting on sofa with arms folded, looking angryLeo tunakamilisha mfululizo wetu wa tatizo la upungufu wa nguvu za kiume kwa kuangalia suluhisho lake.

Tumeona kwamba upungufu wa nguvu za kiume siyo ugonjwa bali ni matokeo ya matatizo yanayotokea mwilini na kuathiri mfumo mzima wa nguvu za kiume.

Matatizo yanayosababisha hali hii tunayagawa katika makundi matatu. Kwanza ni tatizo la kisaikolojia, hapa endapo akili yako haipo vizuri. Pili ni tatizo la kifiziolojia endapo mwili wako haupo vizuri kutokana na uchovu, upungufu wa vichocheo na virutubisho na tatu ni tatizo la kipatholojia kutokana na magonjwa mbalimbali kama kisukari, HIV, magonjwa ya moyo, kansa, kifua kikuu, vidonda vya tumbo, n.k.

Ili uume uweze kufanya tendo la kujamiiana kikamilifu ni lazima uwepo msukumo mzuri wa damu katika uume. Msukumo huu unaweza kuathiriwa na sababu au vyanzo vikuu vitatu ambavyo tumeshakwishaviona. Daktari atamfanyia uchunguzi kufuatana na mambo hayo makuu matatu tulivyoyaona.

JINSI YA KUKABILIANA NA TATIZO

Tatizo la upungufu wa nguvu za kiume linaweza kuanza taratibu au kwa ghafla kutegemea na chanzo, wanaopata tatizo la kisaikolojia mara nyingi tatizo hili huanza ghafla kulinganisha na wengine wenye vyanzo tofauti kama kifiziolojia au kipatholojia kama tulivyoona.

Zipo hatua kumi zinazoweza kukufanya upate mtikisiko katika suala la nguvu za kiume kwa hiyo ukiepuka au ukiachana nazo au hata utazingatia vizuri mafundisho haya utakuwa vizuri na kufurahia ubora wako.

Mambo ya kuzingatia ni kama ifuatavyo: –

Epuka uvutaji wa sigara; sigara ina kemikali zinazosababisha mishipa ya damu inayosambaza damu mwilini kuwa migumu na kushindwa kutanuka kupeleka damu kunakostahili hivyo hata msukumo wa damu katika uume huathirika na uume kukosa nguvu.

Epuka unywaji wa pombe; hakuna utafiti wa kisayansi unaoonesha uywaji wa pombe kali au zisizo kali zinaongeza nguvu za kiume. Unywaji wa pombe unakufanya uwe mchovu, na kushindwa kumudu tendo hata unapomaliza unabaki mchovu. Ulevi pia huharibu figo na mishipa midogomidogo ya fahamu mwilini hivyo kukufanya ukose msisimko unaokusaidia kupata uamsho wa mwili.

Msongo wa mawazo ni vema kuuepuka na kujenga hali ya kujiamini muda wote, watu wenye msongo wa mawazo daima ni watu waliokata tamaa. Hali hii inaweza kukupotezea kabisa uwezo wa kufanya tendo la kujamiiana, hata kama ulishindwa mara ya kwanza ona ni bahati mbaya tu, jitahidi tena baadaye.

Msongo wa mawazo unasababishwa na mambo mengi, yanaweza kuwa kikazi kama umefukuzwa au kusimamishwa, kimasomo, kijamii na kifikra. Epuka msongo wa mawazo na hakikisha unakuwa huru.

Fanya mazoezi ya mwili ili kuwa na stamina na msukumo mzuri wa damu mwilini. Pia yapo mazoezi maalum ya kukusaidia kufanya tendo la kujamiiana kwa ufanisi. Mazoezi haya yanaitwa ‘Kegels exercise’ tutayazungumzia kwa undani katika makala zijazo. Ila mazoezi mengine kama ya ‘Gym’, ‘Jogging’, kucheza mpira na mengineyo ya nguvu husaidia sana kuwa na nguvu za kiume zenye ubora.

Pata mlo bora na wenye afya, ulaji wa matunda na mbogamboga husaidia sana kurutubisha na kujenga nguvu za kiume, kwani huamsha msukumo wa damu na kuufanya uume uwe na nguvu. Vyakula visivyofaa katika mwili wako pia haviwezi kukupa ubora wa nguvu za kiume.

Pata utulivu wa akili na hakikisha mwili na akili yako vipo pamoja na katika hali ya utulivu, pata muda wa kupumzisha akili na mwili baada ya kazi au misukosuko ya maisha kabla ya kujipanga na tendo la kujamiiana na jiepushe kuangalia picha za ngono halafu ndipo ukutane na mwenza wako.

NINI CHA KUFANYA?

Endapo utazingatia mambo yote haya lakini hakuna mafanikio, basi muone daktari wa masuala ya uzazi katika hospitali za mikoa. Huwa hakuna njia ya mkato katika tatizo hili la upungufu wa nguvu za kiume. Tiba yake hupatikana hospitali tu.

Leave A Reply