The House of Favourite Newspapers

Fahamu Madhara Sita ya Kutoa Mimba

KUTOKANA na kuongezeka kwa idadi ya mahusiano duniani na kutotumia njia za uzazi wa mpango kwa watu wengi walioko kwenye mahusiano, wasichana wengi kwa sasa wanatoa mimba.  Zaidi ya asilimia tisini ya wasichana wanaokuwa kwenye mahusiano na wanaume zaidi ya mwaka mmoja kabla ya ndoa, hutoa mimba na asilimia tano tu ya wote ndio wanaamua kuzaa. Sio ajabu kusikia mtu ameolewa akiwa ametoa mimba nne mpaka tano. Hata hivyo hao wanaozaa pia hujikuta wamebeba mimba nyingine wakati watoto wao wakiwa wadogo na kulazimika kuzitoa.

Najua watu wengi wanatoa mimba ili kukwepa aibu, kutokuwa tayari kisaikolojia na kadhalika, lakini ni bora kutumia njia za uzazi wa mpango kama kondomu kwa lengo la kuzuia mimba na kama kondomu huiwezi, basi tumia njia nyingine kama sindano na vijiti kwa sababu wengi wenu mkishalewa pombe au kondomu isipokuwepo, ndio basi tena. Hebu tuyaangalie madhara ya kutoa mimba kama ifuatavyo.

UWEZEKANO MKUBWA WA KUFA

Wanawake wanaotoa mimba wana uwezekano wa kufa mara nne zaidi kuliko ambao hawatoi mimba. Vifo hivyo vimekua vikisababishwa na kujiua wenyewe kutokana na kujuta kwa maamuzi yao na madhara ya muda mrefu ya kimwili yatokanayo na kutoa mimba.

Vifo ndani ya wiki moja baada ya kutoa mimba hutokana na kuvuja damu sana, madhara ya dawa za usingizi, mabonge ya damu kwenye mishipa ya damu na mimba iliyotunga nje ya uzazi. Kutoa mimba moja uwezekano wa kufa unakua 45%, mimba mbili 114%, mimba tatu 192%.

UGUMBA KWA WANAWAKE

Miaka ya hivi karibuni, wanawake wengi ambao wanalia kutopata watoto wana historia za kutoa mimba, miaka iliyopita na wengi wao niliwaona wakijuta sana kwa maamuzi yao. Hii inatokana na madhara makubwa waliyoyapata kwenye mfuko wa uzazi baada ya mimba kutoka.

MIMBA KUTUNGA NJE YA KIZAZI

Mfuko wa uzazi una utando maalumu ambao hufanya mimba iliyotungwa kwenye mirija iitwayo fallopian kuwezesha yai kushuka hadi kwenye mifuko ya uzazi. Lakini utoaji wa mimba huambatana na magonjwa ya mirija hiyo na kupoteza utando huo na kusababisha mimba kukulia huko. Matibabu ya tatizo hili ni kukata mrija husika tu hivyo kuongeza hatari ya ugumba.

KUZAA WATOTO WASIO NA AKILI NZURI

Utoaji wa mimba huharibu mlango wa mfuko wa uzazi kushindwa kushika vizuri na matokeo yake mwanamke hujikuta akizaa kabla ya muda husika akibeba mimba nyingine. Lakini pia watoto hawa wanaozaliwa kabla ya muda maalumu na viungo ambavyo havijakomaa, hupata shida ya ubongo na kuwa wagonjwa wa akili maisha yao yote.

KANSA YA MLANGO WA UZAZI

Wanawake wanaotoa mimba wana hatari kubwa ya kupata kansa ya mlango wa uzazi kuliko wengine ambao hawajatoa mimba. Hii ni kwa sababu ya kusumbuliwa kwa mlango huo kwa dawa za kutoa mimba, vifaa vya kutolea mimba na mabadiliko ya ghafla ya homoni za uzazi.

KUATHIRIKA KISAIKOLOJIA

Hakuna mwanamke ambaye hatakaa ajutie maamuzi yake ya kutoa mimba siku za usoni, hata kama hakupata madhara yoyote. Hii itamfanya aishi kama ana deni fulani maisha yake yote na itakua inamuumiza usiku na mchana.

Nyingine ni kukosa hamu ya kula, kusikia sauti ya mtoto anayelia wakati hayupo, kua na hasira sana. Kumbuka kila mwaka wanawake 70,000 wanakufa kwa kutoa mimba. Maumivu ya kukosa mtoto ni makali sana kuliko aibu ya kuzaa nje ya ndoa.

Kama hutaki mimba tumia njia za uzazi wa mpango. Nenda hospitali watakushauri njia sahihi ya kuzuia kupata mimba kuliko kujiachia na kupata mimba kisha kuitoa. Madhara yake ni mengi na ya hatari kama ulivyoona.

Comments are closed.