The House of Favourite Newspapers

Harmonize Anapata Wapi Jeuri Kujitoa Wasafi

Miongoni mwa majina ya watu maarufu wanaozungumziwa zaidi mwisho wa mwaka 2019, Yupo Harmonize ambaye amekuwa homa kila kona ya mashabiki wa muziki tangu ilipotangazwa kama mmakonde huyo ana nia ya kujitoa kwenye Label ya WCB iliyomtengenezea umaarufu alionao.

 

Haijathibitishwa rasmi kama uongozi wa Wasafi wamekubali kuutengua mkataba wao na Harmonize ambaye amekuwa akiachia kazi zake binafsi na kolabo kadhaa zinazozidi kumuweka kwenye nafasi kubwa ya kusikilizwa kila siku hivyo uwezekano wa muziki wake kufifia itakuwa ndoto.

 

Mitaa imekuwa na mitazamo tofauti kila inapoanzishwa maada ya Harmonize kujiondoa kwenye Label hiyo, yapo makundi yanayomtetea msanii huyo kwa kusema amekua na anao uwezo wa kujitegemea kufanya kazi nzuri, wakati huo huo yapo makundi ambayo yanamtabiria kufeli huku yakisema moja kati ya makosa Harmonize amefanya ni kuondoka WCB Wasafi.
Ukweli ni kwamba Harmonize ni mmoja kati ya watanzania wachache walioamua kuwekeza muda wao mwingi kufanya kazi nzuri zinazomfanya avuke viwango kutokea kuwa msanii hadi mwanamuziki ambaye amejitengenezea heshima kuwa kwenye baadhi ya maeneo ya ndani na nje Afrika.

 

Harmonize alipata nafasi ya kuonyesha mbinu za muziki wake na hakutaka kufanya makosa, amekuwa akiachia nyimbo zinazopata muda mrefu wa kusikilizwa na video zenye mamilioni ya watazamaji kitu ambacho ni ndoto ya wasanii na wanamuziki wengi.
Harmonize anajua kama yeye ni mtu wa aina gani lakini hajui kila mtu anamtafsri kwa namna gani, kitu ambacho anakitumia kama ushawishi wa kutokuwa na chaguo lingine zaidi ya muziki ndiyo sababu amewekeza muda wake mwingi kufanya kazi nzuri na kuzidi kujiboresha kila kukicha.
Hajawahi kulalamika kubaniwa kwenye game wala kuchukua brake ili asubiri mambo yake sawa kitu ambacho kimewapoteza wasanii wengi kwenye ramani ya muziki na kuongeza namba ya manabii ambao wanasema walijua hawafiki mbali, Harmonize siyo mtu wa aina hiyo.

 

Alijijua kama atakuja kuwa mwanamuziki mkubwa na kuyabeba majukumu yake kama mwanamuziki aliyefanikiwa ndiyo maana ameingia kwenye orodha ya wanamuziki wa Afrika ambao kila mwanamuziki wa nchi nyingine anatamani kufanya nae kazi.
Harmonize anafanya kila kitu kuhakikisha thamani ya muziki wake haishuki hata kama atakuwa nje ya WCB. Matukio anayoshiriki yanaonyesha nguvu ya ushawishi wake na wala sio kitu cha ajabu tukimuona mwanamuziki huyu akipata deals na makampuni makubwa.

Harmonize alitambua muziki ndicho kitu kitakachompa mafanikio vikiwemo pesa, umaarufu na heshima. Hakutaka kuishia kuwa msanii wa kulipwa show za laki mbili mpaka milioni moja ambazo zingemsaidia kulipa kodi ya chumba na kuvaa vizuri, alifikiria kujitengeneza brand ya mwanamuziki atakayelipwa pesa nyingi za kigeni kwa kushirikiana na wanamuziki wengine na kufanya matamasha makubwa kwenye nchi za ugenini.

Comments are closed.