The House of Favourite Newspapers

Hawa Ndiyo Wagunduzi wa Virusi Vya UKIMWI

0

Mmoja Atajwa Kuhusika Kuvitengeneza: UGONJWA wa Ukimwi ni hatari na umeua watu wengi sana duniani. Leo tutazungumzia ugunduzi wa ugonjwa huu.

 

Mwanasayansi wa kwanza kutangaza kuwa ameweza kuviona Virusi Vya Ukimwi (VVU) ni mtaalamu wa Kifaransa, Dk Luc Montagnier.

 

Mtaalamu huyo ambaye aliongoza jopo la wanasayansi wengine katika taasisi ya Pasteur ya mjini Paris alitoa ripoti yake katika jarida la sayansi mwaka 1983.

 

Katika utafiti huo alihusisha virusi hao na uvimbe wa kwenye mashavu unaosababishwa na mafindofindo ambayo yalikuwa yanawaandama sana wagonjwa wa Ukimwi.

Hata hivyo, utafiti huo haukuweza kutoa picha halisi ya VVU hadi mwaka uliofuata mwanasayansi wa Kimarekani alipofanikiwa kukielezea kirusi hicho kwa sayansi inayoeleweka zaidi.

 

Mmarekani huyo, Dk. Robert Gallo akiongoza jopo la wanasayansi wengine, mwaka 1984 walitangaza ripoti yao ya utafiti kwa kina na kutoa machapisho manne ya ripoti kwenye jarida la kisayansi. Chakushangaza ni kwamba wapo wanasayansi wanaosema kwamba daktari huyo ndiye aliyetengeneza virusi vya ukimwi.

 

Kwenye jarida hilo alikielezea kirusi kinachosababisha Ukimwi kwa undani na namna kinavyoshambulia mfumo wa kinga.

 

Ripoti hizo baada ya kuchunguzwa zilionyesha wazi kuwa ndivyo ulivyo mfumo wa VVU hivyo mwaka 1986, Dk Gallo akatunukiwa tuzo ya Lasker.

Lasker ni moja ya tuzo za kisayansi zinazoheshimika duniani na ambayo imekuwa ikitolewa kwa watu waliofanya maajabu kwenye fani hiyo.

 

Tuzo hiyo ilimfanya Dk Gallo kupewa heshima ya juu zaidi katika tafiti zilizogundua VVU kuliko zile zilizofanywa na Wamarekani wenzake Dk Paul Volberding na Dk Marcus Conant, mwaka 1981 na ile ya Mfaransa Dk Luc Montagnier, mwaka 1983.

 

Tuzo hiyo ilionekana kumpa kichwa Dk Gallo kwani aliendelea kuchimbua zaidi VVU na kutoa ripoti mbalimbali ziliviweka wazi virusi hivyo na kuwapa picha halisi watafiti wengine duniani.

Moja ya utafiti huo ni ule alioutoa mwaka 1995 ulioonyesha kemikali iitwayo chemokines inaweza kusababisha VVU kushindwa kushambulia CD4 na hatimaye mwili unakuwa haufikii hatua ya kuugua Ukimwi.

 

Kwa namna Dk Gallo alivyoonyesha juhudi za kuchunguza VVU na Ukimwi, Mfuko wa Taasisi ya Bill Gate ilimpa Dola za Marekani 15 milioni sawa na zaidi ya Sh25.5 bilioni mwaka 2007 na hata miaka ya karibuni wameendelea kufadhiliwa.

 

Katika miaka hiyo ya 1980, walijitokeza wataalamu mbalimbali waliodai kuwa na dawa za kukabili Ukimwi.

Wakati huo kukiwa hakuna vipimo vya kubaini VVU, watafiti hao kutoka sehemu mbalimbali duniani, wakiwemo wa dawa za miti shamba, walikuwa wanatibu mtu ambaye tayari amekuwa anaugua Ukimwi.

 

Waliodai kuwa na dawa ni wale waliotibu dalili za ugonjwa kama vile kukonda, ngozi kuharibika, nywele kunyonyoka, vidonda kwenye koo na mdomoni.

Hata hivyo, kutokuwepo na vipimo vya haraka vya kuthibitisha mwathirika kama hana tena VVU, ilikuwa vigumu na mara nyingi walioonyesha kupona walionekana kurejewa tena ugonjwa na hata kupoteza maisha.

 

Mwaka 1985 Taasisi ya Chakula na Dawa ya Marekani (FDA) ilithibitisha kifaa cha kupima uwepo wa VVU kwenye damu.

Kipimo hicho ambacho hadi leo kimekuwa kikitumika ila kwa kuimarishwa zaidi, kwa kawaida kinapi ma uwepo wa chembe kinga maalumu inayotengenezwa na mwili baada ya VVU kuingia mwilini.

 

Kuwepo kwa vipimo hivyo kuliimarisha zaidi watafiti wa dawa kufanya kazi zao kwa uhakika zaidi katika kutafiti.

FDA ilitangaza AZT kuwa ni dawa ya kwanza ya ARV mwaka 1987. Mwaka huo pia ikatangaza aina ya kondomu iliyoimarishwa maalumu katika kuzuia maambukizi pale inapotumika kwa uangalifu.

 

Tangu wakati huo, ARV kadhaa zilitangazwa lakini zilizopo katika kiwango bora zaidi zilithibitishwa kati ya mwaka 1995 na 1996. Nyingi ya dawa hizo zimekuwa zikitumika hadi leo.

Utafiti mwingine umewezesha kuwapo kwa mchanganyiko wa baadhi ya dawa baada ya kuonekana zitakuwa na ufanisi zaidi.

MAKALA: Elvan Stambuli.

Leave A Reply