Inauma Sana… Mama Afia Daraja la Mahita
Daraja la Mahita
Na Dustan Shekidele, Risasi Jumamosi
Morogoro: Inauma sana! Baada ya mwanakijiji mwenzao ambaye ni mama kufa kwa kutumbukia kwenye daraja bovu, baadhi ya waombolezaji wamelala barabarani na kwenye daraja hilo kuzuia uharibifu unaofanywa na malori yanayobeba mchanga.
Tukio hilo lililoibua hekaheka lilijiri katika Kijiji cha Lugala Kata ya Mindu Manispaa ya Morogoro hivi karibuni kwenye Daraja la Mahita lililojengwa kwa msaada wa aliyekuwa Mkuu wa Jeshi la Polisi, IGP Omary Idd Mahita ambaye ni mkazi wa kijiji hicho.
Katika tukio hilo lililoshuhudiwa na mwanahabari wetu, wananchi hao walifikia uamuzi huo baada ya mwenzao kufia darajani hapo akiwa na bodaboda aliyoikodi ambayo ilitumbukia darajani hapo nyakati za usiku na abiria huyo kupoteza maisha papo hapo.
Wananchi hao wakiwa wamelala darajani hapo.
“Ukweli inauma sana, manispaa wanachukua ushuru wa shilingi elfu sita kwa kila lori lakini hawatengenezi daraja.
“Mwanamke mwenzetu amepoteza maisha hivihivi, ilikuwa usiku, akakodi bodaboda ambayo dereva ni mgeni, matokeo yake wakatumbukia darajani na mama wa watu akapoteza maisha huku dereva wa bodaboda akijeruhiwa vibaya,” alisema Asha Shomari, mmoja wa wananchi hao na kuongeza:
“Chanzo cha kuharibika kwa daraja hili ni malori yanayobeba mchanga kutoka kijijini kwetu kwenda mjini ambapo manispaa huyatoza ushuru wa shilingi elfu sita kwa kila gari hivyo wingi wa malori hayo unachangia kuharibu mazingira na kuvunja daraja letu.
“Hivyo leo tumeamua kuandamana na kulala barabarani na darajani ili wahusika wapate ujumbe kwamba tuna hofu na hili daraja.”
Kwa upande wake, Osman Maloto alikuwa na haya ya kusema: “Katika kijiji chetu hatuna shule yoyote wala zahanati hivyo watoto na wajukuu wetu wanasoma Kata ya Chamwino, wanavuka katika daraja hili.
Pia wajawazito wanapita kwenye daraja hili kuelekea Hospitali ya Mkoa wa Morogoro, sasa malori zaidi ya 50 yanayopita kila siku, yamelibomoa daraja hili tulilojengewa na Mahita ndiyo maana linaitwa Daraja la Mahita.”
Baada ya zoezi lao hilo ambalo halikupata majibu ya papo kwa hapo kwa kuwa hakukuwa na viongozi wa serikali, akina mama hao walikwenda kupeleka malalamiko yao kwa mwenyekiti wa kijiji hicho, Sanga Mkulago ambaye alifika eneo la tukio kutatua mgogoro huo kwa busara akisema:
“Kweli kuna tatizo, naomba turuhusu malori yapite chini ya daraja, nitazungumza na mkurugenzi wa manispaa ili kupata suluhisho.”