The House of Favourite Newspapers

JPM anaongoza kupigwa Juju!

0

MagufuliiRais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Pombe Magufuli ‘JPM’

Mwandishi wetu, Amani

DAR ES SALAAM: Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Pombe Magufuli ‘JPM’, huenda ndiye mtu anayeongoza kwa kupigwa juju kwa waganga wa kienyeji kuliko mtu yeyote nchini kwa sasa, Amani linakuja na ushuhuda.

Sangoma mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Shark Abdullah ‘Kishapu’, akipiga simu kutoka jijini Tanga mwanzoni mwa wiki hii, aliliambia gazeti hili kuwa katika miezi ya hivi karibuni, amekuwa akipata wateja, wakiwemo wafanyabiashara na watumishi wa umma wakimtaka kumpunguza kasi ya utendaji kiongozi huyo, wakisema inawaathiri.

BACK---AMANI“Sikiliza ndugu mwandishi, mimi hapa ni mganga wa kienyeji, nataka nikupe habari. Kuna watu wengi sana wanakuja hapa kwangu kutaka niwakinge na tumbuatumbua ya Magufuli, wengine wanataka nifanye ninavyoweza kumfanya asiweze kutekeleza majukumu yake.

“Nimewapokea wafanyabiashara na hata viongozi wakubwa, wanataka utumbuaji wa majipu usiwapitie, wengine wana madhambi ambayo wanataka yasahaulike ili wasalimike, yaani nakuambia hali ni mbaya,” alisema mganga huyo.

Alipoulizwa kama anawafanyia kama wanavyomtaka afanye, alisema anachokifanya yeye ni kuwapa dawa zinazoweza kuwakinga dhidi ya watu wenye nia mbaya kichawi, lakini si kumroga Rais Magufuli.

Madai ya sangoma huyo yanafanana na Shazoe Mustafa, aliyepiga simu miezi michache iliyopita kutoka Bagamoyo, Pwani ambaye alisema vigogo wengi serikalini, wakiwemo wabunge wamekuwa wakienda kwake kwa ajili ya ‘kumchezea’ Rais Magufuli.

“Kuna wabunge fulani walikuja hapa na kusema nifanye ninavyoweza ili rais awape ulaji. Walisema wanataka uwaziri. Yupo kigogo mmoja wa shirika la umma ambaye alikuwa na hofu ya kutumbuliwa, naye akasema niweke ukungu ili Rais Magufuli asione jina lake. Kila anayekuja kwangu siku hizi ana hofu na kutumbuliwa,” alisema Shazoe.

Hata hivyo, wakati waganga hao  wakipata wateja wengi wanaotaka kinga dhidi ya utumbuaji, waumini wa dini zote wamekuwa hawalali, wakisali na kuswali kuomba ili Mwenyezi Mungu amlinde Rais Magufuli, kwa vile kazi yake ni nzito, yenye maadui wengi.

ASKOFU na Nabii Nicolaus Suguye wa Huduma ya Neno la Upatanisho (WRM), Matembele ya Pili- Kivule, Dar aliliambia gazeti hili kuwa wamekuwa wakifanya maombi kila mara kwa ajili ya kumuombea ulinzi Rais Magufuli.

“Mara kwa mara tumekuwa na ibada maalum ya kumuombea rais ili pepo wabaya wakae naye mbali. Tunajua vita anayopigana ni kubwa na hatari, binadamu hawezi kumlinda binadamu mwenzake. Sisi tunataka Mungu ndiye afanye kazi hiyo, ndiyo maana tunakesha kwa maombi,” alisema Nabaii Suguye

Daniel Rashid, Mchungaji wa Kanisa la Assemblies of God, Tegeta naye alisema kwa pamoja, waumini wote wamekubaliana kutenga muda maalum wa kumuombea ulinzi kwa malaika ili waifanye kazi ya kuhakikisha kiongozi huyo mkuu wa nchi anakuwa salama.

“Rais Magufuli anafanya kazi kwa manufaa ya wengi, wachache hawapendi na bahati mbaya, hawa wachache ndiyo wenye nguvu, wako serikalini na mitaani, tunajua hatari iliyo mbele yake, ndiyo maana tunamtanguliza Mungu, ni Mungu tu ndiye anaweza kugeuza mioyo ya wahalifu,” alisema.

Licha ya wachungaji hao, pia viongozi wa Kiislamu kutoka misikiti mbalimbali nchini nao wanadaiwa kutenga muda maalum kwa ajili ya kusoma dua ya kumlinda Rais Magufuli, kwani utendaji wake una faida kwa wanyonge wote wa Tanzania.

Juzi, gazeti hili lilimpigia simu Shehe Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhadi Musa Salum ili kumuuliza kuhusu hilo kwa upande wake lakini simu yake iliita bila kupokelewa.

Leave A Reply