The House of Favourite Newspapers

Kinondoni Kufanya Maonesho ya Ngozi Tanganyika Packers

0
Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Mh Daniel Chongolo akiongea na Waandishi wa Habari katika maandalizi ya maonesho ya bidhaa za ngozi yaliyoandaliwa na Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni yanayotarajiwa kufanyika katika viwanja vya Tanganyika Packers ikihusisha Wafanyabiashara wa bidhaa hizo zaidi ya 100.

 

MKUU wa Wilaya ya Kinondoni, Mhe. Daniel Chongolo amesema kuwa katika kuhakikisha tunakuza uchumi wa Viwanda, Wilaya hiyo imeandaa maonesho ya wajasiriamali wa bidhaa zangozi yatakayofanyika Disemba 12 hadi 15 katika viwanja vya Tanganyika Packers.

 

Akizungumza na waandishi wa habari leo, Mhe. Chongolo amesema kuwa maonesho hayo ambayo yata ambatana na uuzwaji wa bidhaa hizo yatafanyika ikiwa ni katika mkakati wa kutangaza na kuhamasisha wananchi kutumia bidhaa zinazo zalishwa hapa nchini.

 

Amesema kuwa lengo la maonesho hayo ni kutangaza uwezo wa wadau wa ngozi, kuelimisha jamii kujenga utamaduni wa kutumia bidhaa hizo zenye ubora zinazozalishwa hapa nchini sambamba na kuongeza soko la ajira kwa vijana.

 

Amefafanua kuwa katika maonesho hayo yatahusisha wajasiriamali kutoka Wilaya ya Kinondoni pamoja na Halmashauri nyingine zilizo alikwa ikiwemo Ilala, Temeke, Ubungo pamoja na Kigamboni.

 

Mhe. Chongolo amefafanua kuwa kupitia sensa ya mwaka 2012, Manispaa ya Kinondoni inajumla ya wakazi zaid ya milioni 1.3, ambapo idadi hiyo inategemea kupata bidhaa za ngozi, ikiwemo Viatu, Mikanda, Mabegi na pochi zinazo tokana na bidhaa za ngozi.

 

Mhe. Chongolo ameeleza kuwa hali hiyo imekuwa tofauti kutokana na watu hao kutumia bidhaa zinazozalishwa kutoka nje ya nchi na hivyo kuwasihi wannachi kupenda kutumia bidhaa zinazo zalishwa hapa nchini.

 

“Tanzania ni miongoni mwa nchi kubwa barani Afrika zinazo zalisha ngozi kwa kiasi kikubwa , lakini pia Tanzania ni miongoni mwa nchi tatu Afrika zenye mifugo mingi , Tanzania ni Nchi pia ambazo zinatumia bidhaa hizo kwa wingi, mfano rekodi inaonyesha kuwa jumla ya viatu zaidi ya milioni 53 zinaingia na kutumika kila mwaka” ameeleza Mhe. Chongolo.

 

Rais wetu mpendwa, Dk. John Magufuli kila siku amekuwa akisisitiza kujenga viwanda ili kufikia uchumi wa kati, na sisi wasaidizi wake tunaliangalia hilo kwa kulifanyia kazi, ndio mana tumeona tuwaweke pamoja wajasiriamali wa bidhaa za ngozi, na hatutaishia hapa tunampango mwakani tuyafikishe mbali zaidi” amesema Mhe. Chongolo.

 

Serikali ya Viwanda, Mhe. Chongolo amefafanua kuwa pamoja na kwamba Tanzania inazalisha ngozi nyingi lakini ipo changamoto kubwa inayotokana na malighafi hizo kusafirishwa nje ya nchi jambo ambalo amesema limesababisha kuwepo kwa uhaba wa ngozi kwa ajili ya uzalishaji wa bidhaa hizo.

 

Hata hivyo Mhe. Chongolo amesema kuwa kauli mbiu ya maonesho hayo ni Kinondoni yetu, Viwanda vyetu, Tanzania yetu ambapo kupitia maonesho hayo itakuwa ni fursa kwa vijana wengi kujiajiri , kuongeza pamoja na kukuza viwanda vya ndani vya ngozi na hivyo kuongeza uzalishaji na ubora wa bidhaa hizo.

 

Imetolewa

Disemba 10, 2019

Kitengo Cha Habari na Uhusiano Manispaa ya Kinondoni.

Leave A Reply