The House of Favourite Newspapers

Madai: Aliyemuweka Mbongo rehani akamatwa!

0

MBONGO ATESWA-PICHA NA GLOBAL PUBLISHERS (2) Adam Akida Mwinyimkuu aliyetekwa ughaibuni.

Issa Mnally na Elvan Stambuli, UWAZI

DAR ES SALAAM: Mtanzania aitwaye Juma (jina lake la pili tunalihifadhi kwa sababu maalum) anayedaiwa kumuweka rehani ughaibuni Mbongo mwenzake Adam Akida Mwinyimkuu, mkazi wa Magomeni Mapipa jijini Dar es Salaam ambaye ametekwa na kushikiliwa na watu wanaoaminika kuwa ni ‘Wazungu wa Unga’ , amekamatwa na polisi jijini Dar.

sacp mihayoKamanda wa Polisi wa Kikosi cha Kuzuia na Kupambana na Madawa ya Kulevya Tanzania, SACP Mihayo Msikhela

Uchunguzi wa kina uliofanywa na waandishi wetu wiki iliyopita umebaini kuwa, Juma alikamatwa na polisi mwishoni mwa wiki iliyopita Tegeta na anahojiwa kuhusiana na kutuhumiwa kumuweka dhamana kijana Adam kisha kumtelekeza ughaibuni huku ikidaiwa kuwa yeye alikuja na shehena ya unga.

Habari zinasema ili Adamu awe huru, Juma anatakiwa kupeleka fedha shilingi trilioni moja ambazo ni gharama ya unga aliopewa, huku akimfanya mwenzake huyo kuwa ‘bond’ ya mzigo huo haramu.

“Fedha anazodaiwa Juma ni nyingi ni shilingi trilioni moja. Ni kwamba mzigo wenyewe (unga) hakufanikiwa kuuza kwani alikamatwa na askari wakamnyang’anya na sasa sijui atafanya nini ili kumuokoa mwenzake aliye ughaibuni,” kilisema chanzo chetu.

Habari zaidi zinasema kuwa licha ya Juma kuwa korokoroni, baba wa Adamu mzee Akida Mwinyimkuu naye alishikiliwa kwa muda na polisi katikati ya wiki iliyopita lakini hakuwa na msaada wowote kwa vyombo vya dola.

“Mzee Akida alikamatwa na polisi lakini badala ya kusaidia akawa anapotosha ukweli. Yeye aliwaambia polisi kuwa mtoto wake Adam hakwenda Pakistani bali alikwenda Afrika Kusini na ndivyo anavyojua. Alipooneshwa video ya mwanaye akiwa chini ya ulinzi, alishangaa na hakuwa na la kusema,” kilisema chanzo chetu.

Kamanda wa Polisi wa Kikosi cha Kuzuia na Kupambana na Madawa ya Kulevya Tanzania, SACP Mihayo Msikhela (pichani) alipoulizwa na gazeti hili kuhusu kukamatwa kwa mzee Akida na Juma hakukiri wala kukataa.

“Unajua hili jambo bado lipo kwenye uchunguzi, hatuwezi kusema chochote hadi tumalize uchunguzi wetu lakini wote wanaotuhumiwa tunawasaka na tukiwakamata tutawahoji. Tukimaliza upelelezi wetu tutatoa taarifa kwa umma,” alisema kamanda huyo.

Leave A Reply