The House of Favourite Newspapers

Magonjwa yanayoshambulia viungo vya uzazi vya mwanamke!

YAPO magonjwa mengi yanayoshambulia tumbo la uzazi, miongoni mwayo ni ugonjwa ambao ni maarufu kama chango la uzazi.  Ugonjwa huu ni miongoni mwa magonjwa yanayoshambulia viungo vya uzazi vya mwanamke ambapo humsababishia maumivu makali ya tumbo na kushindwa kupata ujauzito, au mimba kuharibika kila zinapoingia.

Zipo aina nyingi mno za chango ambazo zinaweza kujitokeza kila moja peke yake na kwa wakati wake na kusababisha tatizo. Lakini zipo ambazo hujikusanya na kujitokeza kwa pamoja, mkusanyiko huu kitaalamu au kitabibu unaitwa Ovulation Disorder (O.D).

Matatizo haya ya maradhi ya chango la uzazi, hutokana na vifuko vya mayai ya uzazi kitaalamu ovaries kutokuwa na uwezo wa kuzalisha mayai na kufanya yakue kwa wakati muafaka. Mwanamke mwenye matatizo haya hushindwa kuwa na siku za hatari za kunasa ujauzito hivyo kushindwa kuziwinda lakini pia kama zipo basi huwa hazina mpangilio unaoeleweka, hakika hushindwa kuzijua.

Yawezekana mwanamke mwenye tatizo hili akawa na uwezo wa kuzalisha mayai lakini yakashindwa kukomaa au hata yakikomaa yakashindwa kusafiri kwenye mirija ya uzazi kwenda kukutana na mbegu za kiume (sperms) kwa ajili ya kurutubishwa.

Tatizo hili huanzia kwenye ubongo, ambapo sehemu inayohusika na uzalishaji wa homoni hushindwa kufanya kazi yake vizuri na hivyo kushindwa kudhibiti uzalishaji wa homoni za Follicle Stimulating Hormone (FSH) na zile ziitwazo Lutenizing Hormone (LH) ambazo ndizo zinazohusika na uzalishaji na uchavushwaji wa mayai ya mwanamke katika viungo vyake vya uzazi.

Wanawake wavutaji wa sigara waelewe kwamba matumizi ya tumbaku ni miongoni mwa sababu zinazotajwa kusababisha homoni za mwanamke kuvurugika na hivyo kupata tatizo hilo. Kuziba kwa mirija ya uzazi, maambukizi katika via vya uzazi na kufunga kwa shingo ya kizazi ni sababu nyingine za tatizo hili.

Chanzo kingine cha tatizo hili ni Hyperplo-lactinemia ambapo mwili wa mwanamke huzalisha homoni ya Prolactin kwa wingi ambayo ikizidi katika damu, huzuia uzalishwaji wa homoni nyingine ya Oestrogen ambayo hutumika kuchochea uzalishaji wa mayai ya uzazi. Wanawake wenye uzito mkubwa wapo kwenye hatari kubwa zaidi ya kupatwa na chango la uzazi.

DALILI ZA CHANGO LA UZAZI

Dalili za chango la uzazi kwa mwanamke ni pamoja na kupata maumivu makali wakati anapokaribia kuingia katika siku zake za hedhi, kuhisi maumivu makali wakati wa kushiriki tendo la ndoa, kujisikia homa kali anapokaribia siku zake za hedhi pamoja na kujisikia uchovu mkubwa anapokaribia siku zake za hedhi.

Pia kuvurugika kwa mzunguko wa hedhi ni dalili nyingine ambapo mwanamke anaweza kuwa na mzunguko mrefu wa hedhi wa takriban siku 35, kubadilikabadilika kwa siku za hedhi au kuwa na mzunguko mfupi wa hedhi chini ya siku 21.

Dalili nyingine ni mwanamke kuwa na hasira kali anapokaribia kuingia katika siku zake za hedhi, kupata michubuko sehemu zake za uke, kuchukia kushiriki tendo la ndoa, kupata uvimbe kwenye kizazi na mimba kutunga nje ya mfuko wa uzazi.

MADHARA YAKE

Yapo madhara mengi kwa mwanamke mwenye tatizo hili lakini kubwa, huwa ni vigumu kupata ujauzito na hata pale anaponasa ujauzito, huharibika na kutoka kwa rahisi. Pia mwanamke kushindwa kufurahia tendo la kufika kileleni wakati wa tendo.

MATIBABU

Tatizo hili huwa halina dawa za moja kwa moja zinazoweza kutibu hospitalini, zilizopo nyingi huwa ni za kurekebisha mfumo wa homoni mwilini, kama mwanamke amepata uvimbe, atapewa dawa za kuondoa uvimbe huo au kufanyiwa upasuaji na kama anapata maumivu makali kabla na wakati wa hedhi, atapewa dawa za kumaliza tatizo hilo.

Comments are closed.