Mambo 6 Ya Kuyazingatia Kabla Ya Kuanza Biashara 2019
TUNAPOELEKEA kuuanza mwaka mwi ngi n e wa 2019, nina uhakika nyote mnatambua kuwa kuna umbali mkubwa kati ya wazo zuri na mwanzo mzuri. Lakini watu wengi hawajui namna kujenga daraja kuziba pengo hilo. Watu wamefeli kwenye biashara zao waliozoanzisha kwa sababu hawakutafakari vya kutosha juu ya vitu vya muhimu vya kuzingatia kabla ya kuanza.
Leo, nataka nikushirikishe vitu vya mhimu ambavyo unapaswa kuvizingatia kabla ya kuingia kwenye biashara kama namna ya kujiajiri hasa tunapouanza mwaka 2019;
UKO TAYARI KWA AJILI YA MAISHA YA BIASHARA INAYOANZA?
Kama kwa sasa wewe ni mwajiriwa wa kampuni nyingine, kuanza ya kwako kama mjasiriamali ni staili mpya ya maisha. Usifanye kosa la kufikiri kuwa hii ni namna ya kupata utajiri haraka au kuyakimbia matatizo yako yote.
Kuanza biashara mpya ni kazi ngumu, inahitaji dhamira ya dhati na kujifunza, na huwezi kuona matunda yake mpaka muda mrefu upite. Jitathmini na uwe mkweli kabla hujakurupuka.
JE, KUNA WATEJA KWELI WENYE UHITAJI NA WENYE PESA?
Kule kushawishika kwako kama unalipenda wazo, kila mtu atapenda huduma ni muhimu, lakini haitoshi. Wateja wanaweza ‘kuipenda’ bidhaa. Lakini kwa kawaida watalipia vitu vile tu ambavyo ‘wanavihitaji’, kimwili au kihisia. Au watu wale ambao ni wahitaji hasa wa bidhaa yako, hawana pesa. Zungumza na wataalam katika sekta yako, pata muda wa kuzungumza na wafanyabiashara wazoefu au wale ambao wamekuwa kwenye sekta hiyo kwa muda wa kutosha ili ujifunze kutoka kwao juu mahitaji yalivyojificha au changamoto zilizojificha.
JE, SOKO NI KUBWA NA LINAKUA?
Kwa mara nyingine tena, usiamini mawazo yako na shauku yako peke yake katika jambo hili. Tafuta taarifa za masoko kutoka kwa watu wa kuaminika ambao hawahusiki na biashara yako. Yaani kampuni inayofahamika kitaifa katika masuala ya utafiti wa masoko. Kadiri unavyopata takwimu za kuaminika ndivyo unavyopaswa kujiamini zaidi. Uwezekano wa soko kukua katika sekta unayotaka kuingia, inapaswa kuwa ni ishara nzuri na kwa upande mwingine kama soko hilo linashuka, basi hiyo iwe ishara njema kwako usichukue hatua za haraka.
JE, BIASHARA YAKO INA UTEGEMEMEZI AU GHARAMA ZILIZOJIFICHA?
Bidhaa nyingi zinashindwa kufanya vizuri kwa sababu ya ‘utegemezi’ na gharama zilizojificha. Katika kila biashara kuna gharama zilizojificha ambazo mara nyingi hutaziona hadi uwe makini sana. Kwa bahati mbaya, watu wengi watakaokutia moyo kuingia katika biashara, wao huwa hawazishiriki gharama hizo zilizojificha. Kabla hujapiga hatua zaidi jiulize ni gharama zipi zimejificha kwenye biashara unayotaka kuingia? Hakikisha unazielewa gharama zote, njia zote za mauzo, mahitaji ya kulifikia soko, na masuala yanayohusiana na utamadumi.
JE, UMEZIANGALIA GHARAMA KATIKA UHALISIA WAKE?
Wajasiriamali wenye shauku sana wana kawaida ya kutengeneza michanganuo ya biashara yenye rangi za uwaridi, kukuza makadirio ya mauzo siku za awali na kushusha makadirio ya gharama. Ili kubadilisha shauku yako iwe biashara hai, andika mchanganuo wa biashara ambao utatoa picha halisi ya kifedha na umpatie mtaalam aukague.
JE, UNA USTAHIMILIVU NA MAARIFA?
Kama mwanzilishi, siku zote mzigo wa majukumu utarudi kwako. Hakuna nafasi ya kuhamishia lawama kwa mtu mwingine. Pamoja na sababu nyingine kuhusika, biashara nyingi mpya zinashindwa kwa sababu ya kukata tamaa na si kwa sababu ya kukosa pesa au muda. Tilia mkazo kujijenga kuwa mtu mwenye usitahimilivu, jifunze kwa bidii na endelea kujiongeza. Kama umewahi kuwa na matatizo na makampuni mengi, inawezekana ukawa sehemu ya tatizo.
na Mwandishi Wetu
Comments are closed.