The House of Favourite Newspapers

Mambo ya kuzingatia kabla ya kuwa mjamzito

0

pregnant_2176694b.jpgUjauzito ni safari ndefu inayomchukua mwanamke miezi tisa au majuma arobaini hadi kujifungua. Ni safari yenye mikikimikiki na hatari nyingi kwa mama na mtoto. Tusichukulie suala la ujauzito kama jambo la kawaida ingawa pia ni wajibu kwa mwanamke.

Ujauzito siyo hali ya hatari au kutisha endapo mambo ya msingi yatazingatiwa kabla ya kuwa mjamzito na kipindi cha ujauzito hadi baada kujifungua. Katika kipindi cha ujauzito kuna mambo mengi ambayo ni mabadiliko humtokea mama na mtoto aliye tumboni.

Katika makala haya tutazungumzia mambo ya kuzingatia kabla ya kuamua kubeba mimba, siyo kila mwanamke anaweza kubeba mimba kwa sababu wengine huwa na matatizo katika mfumo wao wa uzazi, aidha homoni zao hazifanyi kazi vizuri na mayai hayazalishwi au hayapevuki. Huenda pia mirija ya uzazi imeziba au ana matatizo ndani ya kizazi.

 

NINI CHA KUFANYA?

Ni vyema upange sasa unataka kuwa mjamzito au mwezi fulani unataka kushika mimba, uwe na mpango. Hata hivyo, hakikisha umri wako upo zaidi ya miaka 20 kwa usalama zaidi wa afya yako. Mshirikishe mwenzi wako na mwambie ungependa upate ujauzito, siyo vizuri kushtukiza kwani inaweza kukupa ‘stress’ wewe mwenyewe au mwenzako endapo mmoja wenu hajajiandaa kisaikolojia.

 

CHEKI AFYA YAKO

Hakikisha una afya njema, huna magonjwa sugu kama kisukari, shinikizo la damu, magonjwa mengine ya moyo, kansa, HIV, kifafa, pumu, sikoseli au grupu lako la damu ni RH negative. Endapo una matatizo hayo hapo juu, basi haraka wasiliana na daktari wako wa masuala ya uzazi akupe ushauri kwani magonjwa mengine yatakusumbua wakati wa ujauzito, au magonjwa yenyewe yatamwathiri mtoto. Hakikisha huna magonjwa au matatizo katika viungo vya uzazi, mfano kutokwa na uchafu ukeni wenye muwasho na harufu mbaya, vipele au vidonda sehemu za siri, maumivu wakati wa tendo la ndoa, kutokwa na damu au usaha ukeni. Vilevile mfumo wako wa uzazi uwe vizuri, matatizo katika mfumo wa uzazi ni kama vile maumivu ya tumbo chini ya kitovu, kuvurugika kwa mzunguko wa hedhi, kutopevusha mayai na kukosa hamu ya tendo la ndoa.

 

VILEVI ACHA

Epuka unywaji wa pombe na uvutaji wa sigara, hili hata kwa mwanaume anayetaka mtoto. Mwanamke kabla ya kuwa mjamzito hakikisha unakula sana mboga za majani ili upate kiwango kizuri cha vitamin ya Folic Acid, vema ule sana mboga za majani au upate virutubisho vya Folic Acid. Endapo hutakuwa na kiwango kizuri cha Folic Acid, kuna hatari ya kuzaa watoto wenye matatizo.

 

MAZOEZI

Fanya mazoezi mepesi mara kwa mara ili kuimarisha nyonga na viungo vyako vingine na usipate matatizo wakati wa kujifungua. Pata ushauri wa daktari kipindi muafaka.

 

YANAYOKWAMISHA UJAUZITO

Matatizo yanayoweza kukusababishia usipate mimba ni kutofahamu siku za kupata mimba, kuziba mirija ya uzazi.Pia uwepo wa uvimbe ndani ya kizazi na kwenye vifuko vya mayai. Uvimbe wa aina hii unaweza kutibika kwa dawa na ukaisha au kwa njia ya upasuaji, inategemea na daktari wako atakavyoona na kuamua. Kwa upande wa wanaume wanaojiandaa kuwa wazazi ni vema umjulishe mpenzi wako sasa unataka mtoto au lini unataka mtoto.

Ni vema mume na mke kabla ya kuamua kuzaa mkapime afya zenu ili kubaini kama mna matatizo.

Leave A Reply