The House of Favourite Newspapers

Matatizo Ya Uzazi Kwa Wanawake

0

ovariancystdiagram.jpgKama tulivyoona wiki iliyopita, matatizo ya uzazi kwa wanawake yapo katika makundi matatu.

Kuna tatizo la upevushaji mayai. Tatizo hili kitaalamu linaitwa ‘Ovulatory Factor’, husababishwa na kasoro mbalimbali kwenye mfumo wa homoni ambao hutokana na uwepo wa uvimbe katika ubongo, kuwa na upungufu katika mfumo wa homoni, uvimbe wa vifuko vya mayai, vifuko vya mayai kushindwa kuzalisha vichocheo au mayai yenyewe, kuchelewa kwa mwili wa mwanamke kupevuka na magonjwa mbalimbali pamoja na unene kupita kiasi.

Matatizo haya huambatana na dalili mbalimbali, kutegemea na jinsi tatizo linavyotokea, mfano kutokuota vinyweleo sehemu za siri na kwapani, kutokuota matiti au kuchelewa kupata mabadiliko hayo. Kuota ndevu na vinyweleo mikononi na miguuni, hata tumboni na kifuani kwa wanawake. Kutokupata damu ya hedhi kabisa au kufunga kupata kwa muda mrefu.

Matiti kutoa majimaji au maziwa, kupoteza hisia na raha ya tendo la kujamiiana. Kwa hiyo mwanamke anaweza kuwa na zote au mojawapo ya dalili hizo kutegemea na athari zilizojitokeza kwake.

Kuna matatizo ya nyonga ambayo yapo chini ya tumbo usawa wa kitovu ni mojawapo ya matatizo makubwa yanayoathiri uzazi kwa mwanamke.

Lakini maambukizi mbalimbali, mfano ugonjwa wa kidole tumbo ambao wengi wamezoea kuita “Apendix’ lakini kitaalamu unaitwa ‘Appendicitis’ huweza kusababisha mwanamke kuwa na maumivu makali tumboni.

Maambukizi sugu katika viungo vya uzazi au ‘PID’, kushikamana kwa kizazi kutokana na makovu yanayosa-babishwa na kusafisha kizazi mara kwa mara na baada ya mimba kuharibika au kudhani kwamba ni msaada wa kuharakisha kupata mimba, kasoro katika tabaka la ndani la kizazi kuwa nje ya kizazi, uvimbe wa fibroid pia huchangia kwa kiasi kikubwa ugumba.

Dalili

Dalili kuu za matatizo haya ni maumivu sugu chini ya tumbo, kuvuruga mzunguko wa hedhi au kutokupata hedhi, maumivu wakati wa tendo la kujamiiana, kutokwa na uchafu ukeni kwa muda mrefu wenye muwasho na harufu.

 Mwanamke anaweza kuwa na tatizo katika shingo ya kizazi na tatizo hili linaweza kuwa la kuzaliwa nalo, likasababishwa na matumizi ya baadhi ya dawa kwa mjamzito, hivyo kumfanya kuzaa mtoto mwenye kasoro katika viungo vyake mojawapo ni viungo vya uzazi.

Mwanamke anaweza kupata tatizo la uzazi kutokana na kufanyiwa upasuaji au magonjwa sugu katika uke au shingo ya uzazi.

Ukizungumzia tatizo la ugumba kwa mwanaume na mwanamke lazima kuwepo na uchunguzi wa kidaktari ili kugundua. Kwa mwanamke mambo ya kuangalia ni historia yake katika matumizi ya madawa ya tiba, alipokuwa mdogo au hata kama mama yake aliwahi kutumia aina fulani za madawa wakati wa ujauzito.

Daktari ataangalia alivunja ungo kwa wakati muafaka, mfano aliwahi sana au alichelewa sana. Muda muafaka ni kati ya miaka 11, 12 hadi 16. Kufahamu mzunguko wake wa hedhi unavyoenda na kiwango cha damu unachopata, kama alishawahi kutumia njia za kisasa za uzazi wa mpango au alishawahi kuzaa au kuharibu mimba.

Vilevile inahitajika kujua kama ulishawahi kufanyiwa upasuaji wowote chini ya tumbo mfano kutoa uvimbe, mimba nje ya kizazi, kuzaa mtoto kwa upasuaji. Ni muhimu pia daktari akafahamu endapo ulishawahi kupata maambukizi yoyote katika viungo vya uzazi.

Tatizo hili la kutokupata mtoto au ugumba kama tulivyokwishaona hapo awali, linawahusu mke na mume, yaani watu wawili wanaotafuta mtoto lakini mimba ama zinatoka au hafanikiwi kabisa.

Kwa hiyo, mwanamke mwenye tatizo hili la kutopata ujauzito anatakiwa kwenda kuonana  na madaktari bingwa wa matatizo ya uzazi na atafanyiwa vipimo vya kisayansi. Ni vema kwenda wote wawili kufanyiwa vipimo.

Leave A Reply