Mramba, Yona wazua tafrani
Waliovaa ‘ovaroli’ ni Mawaziri wa zamani, Daniel Yona (kulia) na Basil Mramba (kushoto) wakikabidhiwa vifaa vya kufanyia usafi katika Hospitali ya Sinza , Palestina, Dar.
Denis Mtima na Chande Abdallah, Risasi Mchanganyiko
DAR ES SALAAM: Mawaziri wawili wa zamani, Daniel Yona na Basil Mramba waliohukumiwa jela miaka mitatu kabla ya kupunguziwa adhabu na kutakiwa kufanya kazi za kijamii, mwanzoni mwa wiki walizua tafrani kubwa walipotokeza katika Hospitali ya Palestina iliyopo Sinza jijini Dar es Salaam ili kuanza kutumikia hukumu hiyo.
Njemba (hakufahamika jina lake mara moja) akizungumza kwa msisitizo kuwataka Mramba na Yona wafanye usafi huku wananchi wakiwashuhudia.
Mmoja wa watu waliokuwa eneo hilo ambaye hakutambulika jina lake mara moja ndiye aliyekuwa chanzo cha tafrani hiyo kwani mara baada tu ya kuona gari la wafungwa hao, alipaza sauti akiwataka washuke haraka waanze kufagia ili raia washuhudie kama ni kweli.
Njemba huyo akijipenyeza na kuingia kwenye ofisi za hospitali hiyo ili kuwakabidhi Yona na Mramba mfagio.
“Tunataka washuke wakafagie ndiyo tujue kama kweli maana naona kama wanacheleweshwa,” alisikika akizungumza kwa sauti jamaa huyo ambaye baadaye alitolewa nje na walinzi baada ya kuzidisha vurugu.
Mawaziri hao walichukua takriban dakika nane wakiwa ndani ya gari walilokuja nalo wakifikiria namna ya kushuka kwani umati mkubwa uliwazunguka, baadaye walishuka na kuongozwa na Afisa Huduma za Jamii Wilaya ya Kinondoni, Deogratius Shirima hadi kwenye chumba maalumu kwa ajili ya kupewa maelekezo.
Tafrani ikiatokea baada ya mlinzi kumzuia njemba huyo.
Akizungumza na waandishi wa habari hospitalini hapo, Shirima alisema siku hiyo (Jumatatu) ilikuwa ni ya kuwapa maelekezo namna ambavyo watafanya usafi ili jana waanze rasmi kutumikia adhabu yao.
Naye Afisa Mazingira wa hospitali hiyo, Miriam Mongi aliwakabidhi Yona na Mramba vifaa vya kufanyia usafi ambavyo ni mifagio, mafyekeo, viatu maarufu kama ‘gambuti’ na glovu.
Oktoba 2, 2015 katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, hukumu ya rufaa dhidi ya mawaziri hao wastaafu ilitoka, ambapo Jaji Projest Rugazia, alikubaliana na hoja kwamba kwa mujibu wa mashtaka yaliyowatia hatiani, ya matumizi mabaya ya ofisi na kwa mujibu wa kifungu cha 35 cha adhabu, ambacho mahakama ilikitumia, walipaswa kupewa adhabu ya kutumikia kifungo cha miaka miwili na si miaka mitatu.
Mawaziri hao wa zamani waliwasilisha barua hiyo ya kuitaarifu mahakama yenye kumbukumbu namba 151/DA/3/11/223 ya Desemba 5, mwaka jana, wakiongozwa na jopo la mawakili wao watatu Peter Swai, Cuthbert Nyange na Elisa Msuya ndipo hivi karibuni baada ya mahakama kupitia upya kesi hiyo ikaamuru wapewe adhabu ya kifungo cha nje huku wakifanya kazi za kijamii kwa muda wa saa nne kila siku kwa miezi sita.
Mramba aliwahi kuwa Waziri wa Fedha na Yona alikuwa Waziri wa Nishati na Madini katika serikali ya awamu ya tatu chini ya Rais Benjamin Mkapa