Nahodha wa Timu ya Soka ya Brazil Afariki Dunia
Aliyewahi kuwa nahodha wa timu ya taifa ya soka ya Brazil, Carlos Alberto Torres amefariki dunia jana Oktoba 25, 2016 akiwa na umri wa mika 72 baada ya kusumbuliwa na tatizo la shinikizo la moyo.
Carlos Alberto aliyezaliwa Julai 17, 1944 ndiye aliiongoza Brazil kushinda ubingwa kwenye fainali za Kombe la Dunia za mwaka 1970 zilizofanyika nchini Mexico baada ya kuifunga Italia kwenye mechi ya fainali iliyopigwa kwenye Uwanja wa Azteca jijini Mexico City.
Katika mechi ya fainali dhidi ya Italia mwaka huo, Carlos Alberto alifunga bao maridadi baada ya kuwachenga mabeki na kufunga kwa mkwaju mkali bao ambalo liliwekwa historia na kuingizwa kwenye rekodi ya dunia ya mabao mazuri zaidi kuwahi kufungwa kwenye fainali hizo.
Carlos Alberto (wa kwanza kushoto, waliosimama) aliifungia Brazil mabao 8.
Katika kikosi cha Brazil cha mwaka 1970 kilichochukua ubingwa huo, kilihesabika kuwa kikosi bora zaidi cha timu ya taifa kuwahi kutokea duniani ambapo kilijumuisha wakali kama Pele, Jairzinho, Tostao na Rivelino.
Alberto alitajwa kwenye Kikosi cha Soka cha Dunia cha Karne ya 20 mnamo mwaka 1998 na kuwa miongoni mwa wachezaji soka 100 wa Fifa waliohai mwaka 2004.
Baada ya kustaafu kucheza soka akiwa huko Amerika ya Kaskazini na timu ya New York Cosmos, aliweza kufundisha vilabu takribani 13 vikiwemo vya Oman na kumalizia Azerbaijan mwaka 2005.
Wakati wa enzi za uhai wake, Carlos Alberto aliwahi kushinda makombe ya nyumbani mengi akiwa na vilabu vya Santos na Fluminense ambavyo alivichezea mechi 400.
Carlos Alberto atakumbukwa kwa kufunga moja ya magoli bora katika historia ya kombe la dunia, mnamo mwaka 1970.
Comments are closed.