The House of Favourite Newspapers

Polepole Awatolea Povu Upinzani ‘Walisubiri Oil Chafu’

KATIBU wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Humphrey Polepole, , amesema kinachowatesa vyama vya upinzani nchini ni uchaguzi kuugeuza sherehe badala ya kufuata kanuni.

 

Ametoa kauli hiyo leo tarehe 7 Novemba 2019, kuhusu malalamiko yanayoelekezwa kwa chama hicho kwamba kina mkono katika kuenguliwa kwa wagombea wa upinzani.

 

“Uchaguzi huu unafuata sheria na kanuni, wenzetu walijua uchaguzi ni shamrashamra, hawakuwekeza…,” amesema Polepole na kuongeza: “Wenzetu wengi walijua unaingia tu na wengine hawakuwa na michakato kabisa.”

 

Akizungumzia malalamiko ya vyama vya upinzani, Polepole amesema vyama hivyo havikujitayarisha kwa kuwa, vilikuwa vikisubiri wagombea wa CCM waliotemwa ili ‘wawabebe’ kwenye uchaguzi huo.

 

“Walikuwa wakikaa kimya kwa sababu walizoea mgombea wa CCM ambaye hakupata uteuzi, wanamchukua na kumfanya mgombea wao. Wanasubiri kama fisi kuangalia mkono unarudi nyuma kama unadondoka chini, halafu wao wakapate wagombea.”

 

Amevinanga vyama vya upinzani, kwamba kwenye chaguzi zote, vimekuwa vikishindwa kujiandaa na michakato ya ndani na badala yake, vimekuwa vikichukua wagombea wabovu wa CCM.

 

“Tunawezaje kuwa na vyama ambapo kwenye chaguzi zote wanategemea wagombea wabovu, walioshindwa kwenye Chama Cha Mapinduzi ili wakawe wagombea wao?” amehoji.

 

Akielezea kile kilichosababisha wagombea wa CCM kufanya vizuri katika ujazaji fomu, Polepole amesema ndani ya chama hicho, kuna utaratibu maalum.

 

Na kwamba, chama hicho kilituma wanasheria na mawakili wake nchi nzima kukagua na kujiridhisha kuwa fomu zinazojazwa zinakosa kasoro yoyote.

 

“CCM ilituma mawakili na wanasheria 1,250 kote nchini Tanzania. Timu ya mawakili na wanasheria tuliwagawa kiwilaya, wakawa wanashuka kwenye kata moja kwenda nyingine kukaa na wagombea wa CCM kuwapatia msaada wa kisheria, wa namna ya kujaza nyaraka zote zinazohusika na fomu.

 

“Hatukuruhusu mgombea mmoja wa CCM ajaze fomu nyumbani kwake na mkewe au mumewe bila ya wakili na mwanasheria wa chama kukaa naye na kujiridhisha kama taarifa zote zilikuwa sawasawa.”

 

Amesema, chama hicho kilijipanga kuomba dhamana kwa Watanzania, hivyo kilikuwa na kila sababu ya kujiandaa na kujipanga.

 

“Tarehe 29 wote tulichukua fomu, tukajaza na mawakili na tukazirejesha,… sisi tulijipanga kuomba dhamana kwa Watanzania, imeonesha umakini wa kiwango cha juu kwa chama chetu cha Mapinduzi,” amesema.

Comments are closed.