The House of Favourite Newspapers

Safu Mpya Yanga Balaa!

KAMATI ya Utendaji ya Yanga chini ya Mwenyekiti wake, Dk. Mshindo Msolla imeunda kamati mpya ya Mashindano yenye wajumbe 13 chini ya Mwenyekiti, Rodgers Gumbo na bosi wa Kampuni ya GSM Injinia Hersi Said.

 

Hiyo yote katika kuelekea mchezo mkubwa wa watani wa jadi kati ya Simba na Yanga utakaopigwa Januari 4, mwakani kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

 

Timu hiyo imetangaza kamati hiyo mpya ikiwa ni siku chache tangu ivunjwe pamoja na Benchi la Ufundi la timu hiyo lililokuwa chini ya kocha wake Mkongomani, Mwinyi Zahera aliyesitishiwa mkataba kabla ya Charles Boniface Mkwasa kukaimu nafasi yake.

 

Kwa mujibu wa taarifa ambazo imezipata Championi Jumatano, wajumbe hao tayari wameanza kazi hiyo ya kuiongoza timu hiyo wakijiandaa na mchezo wa ligi dhidi ya Alliance United utakaopigwa keshokutwa Ijumaa kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.

 

Kwa mujibu wa taarifa rasmi ya klabu, wajumbe hao 13 wanaounda kamati hiyo mpya kuwa Injinia Hersi Said, Beda Tindwa, Thobias Lingalangala, Edward Urio, Max Komba, Salum Mkemi, Yossuphed Mhandeni, Yanga Makaga, Adonis Bitegeko.

 

Wengine ni Injinia Heriel Mhulo, Injinia Isaack Usaka, Injinia Deo Muta na Hassan Hussein ambao wao kazi yao pekee ni kuweka mikakati ya timu kupata matokeo mazuri katika michezo ya ligi na mashindano mengine.

 

Mmoja wa viongozi wa Yanga aliongeza kuwa kamati hiyo itashirikiana kufanya kazi pamoja na Kamati ya Ufundi inayoongozwa na mwenyekiti wake, Salum Rupia ambaye aliwahi kuwa mwenyekiti wa usajili msimu wa 2010/ 2011.

 

“Ilikuwa ni lazima tuifanyie marekebisho kamati yetu ya mashindano kwa kuhakikisha wanakuwepo watu wenye uwezo wa kuisimamia timu ili kuhakikisha wanafanikisha ushindi kwenye kila mchezo wetu wa ligi na mashindano mengine.

 

“Tunashukuru tayari viongozi wa kamati hiyo wamepatikana na tunachosubiria ni kuona timu ikipata matokeo mazuri ya michezo yetu ya ligi na mashindano mengine.

 

“Kikubwa tulikuwa tukitaka kuona timu inapata matokeo mazuri na hayo yanapatikana pale morali ya timu inapokuwa kubwa inasaidia wachezaji kupambana uwanjani na kufanikiwa kupata ushindi,”alisema mtoa taarifa huyo.

 

Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano wa Yanga, Hassani Bumbuli amesema : “Ni kweli tayari imeteuliwa kamati iliyoanza kazi yake mara baada ya kupewa majukumu hayo na kikubwa tunataka kuona mafanikio zaidi siku za mbeleni.

 

Wilbert Molandi, Dar es Salaam

Comments are closed.