Vitambulisho Vya Taifa: Watumishi wa Umma Mwisho Kujisajili Oktoba 31
Nchemba akipokea maelezo ya namna shughuli za usajili zinavyo ratibiwa.
Agizo hilo limetolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mh. Angellah J. Kairuki (Mb) alipozungumza na waandishi wa habari mjini Dodoma, katika mkutano wa pamoja ulioitishwa kati ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na Waziri ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.
Bi Kairuki amesisitiza; “waajiri na watumishi watakaoshindwa kutekeleza zoezi hili watachukuliwa hatua stahiki kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu zilizopo”
Akifungua mkutano huo uliolenga kutoa tathmini ya mwenendo wa zoezi linaloendelea la Usajili wa Vitambulisho vya Taifa kwa Watumishi wa Umma lilioanza nchi nzima tangu Oktoba 03, 2016, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mh. Mwigulu L. Nchemba (Mb) amesema mpaka sasa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) imefanikiwa kusajili zaidi ya asilimia 50% ya watumishi wote nchi nzima na baadhi ya mikoa kukamilisha usajili kwa zaidi ya asilimia 95%. Ameutaja mkoa wa Geita kuwa mkoa unaoongoza kwa kufanya vizuri katika zoezi hilo
Amesema pamoja na kuwepo kwa changamoto mbalimbali zilizokwamisha zoezi hilo kukamilika kwa wakati uliopangwa; Wizara yake kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma, wameamua kuongeza muda wa kukamilisha zoezi hilo kwa wiki mbili zaidi hadi Oktoba 31, 2016.
Amewataka watumishi kuondokana na upotoshwaji unaofanywa na baadhi ya watumishi kwamba zoezi hilo limelenga kuhakiki vyeti na badala yake wajitokeze kwa wingi kusajiliwa kwani Serikali imelenga kuunganisha taarifa za mfumo wa mishahawa wa Serikali na NIDA, ili mbali na kutatua tatizo la watumishi hewa; kupitia mfumo huu wa kielektroniki unaomtambua mtu kwa alama zake za kibaiolojia kuwa na maslahi mapana kwa taifa na kwa watumishi; kwa kuunganisha mifumo mingine ya Serikali ukiwemo mfumo wa Kodi, mifuko ya Hifadhi za Jamii, Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu, Bima ya Afya, Uhamiaji, RITA Na Benki ili kutoa manufaa mapana kwa mtumishi.
Amelipongeza Jeshi la Wananchi wa Tanzania kwa kuwezesha kusambazwa kwa vifaa vya usajili nchi nzima, Ofisi ya Rais TAMISEMI, Taasisi na Mashirika yote ya Serikali waliojitoa kufanikisha zoezi la Usajili.
Kupitia zoezi la Usajili Watumishi wa Umma, Tayari NIDA imefungua ofisi za usajili nchi nzima, ngazi ya Wilaya kusogeza karibu zaidi huduma inayotolewa kwa wananchi. Kwa mujibu wa Waziri Mwigulu Pindi zoezi la usajili watumishi litakapokamilika usajili wa wananchi utaanza mara moja nchi nzima kwani zoezi la usajili vitambulisho vya Taifa limelenga kila mwananchi, Mgeni anayeishi kihalali nchini na Mkimbizi.
Comments are closed.