The House of Favourite Newspapers

Simba hatari, yashinda mechi ya sita mfululizo

0

Simba-Day-559x520Wachezaji wa Simba wakishangilia goli.

Johnson James, Shinyanga
SIMBA ni hatari! wala huwezi kubisha kwa hilo baada ya kufanikiwa kuichapa Kagera Sugar bao 1-0 kwenye mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, uliopigwa katika Uwanja wa Kambarage, jana.

Simba sasa haijapoteza kwenye michezo yote ambayo imecheza chini ya kocha mpya wa timu hiyo, Jackson Mayanja, ukiwa ndiyo mchezo ambao uliaminika kuwa unaweza kuwa kizuizi kwa timu hiyo ya Msimbazi.

Hii imeonyesha kuwa Simba ndiyo timu ambayo inaweza kuwa na nafasi kubwa ya kutwaa ubingwa baada ya kucheza michezo sita (ukiwemo wa Kombe la FA) mfululizo na kufanikiwa kushinda yote.
Ilianza kwa kuichapa Mtibwa 1-0, JKT Ruvu 2-0, Burkina Faso 3-0 (Kombe la FA), African Sports 4-0, Mgambo 5-1 na mchezo wa jana.

Simba ambao awali chini ya kocha Dylan Kerr walionekana kuwa nyanya walijipatia bao lao kupitia kwa Ibrahim Ajib, ambaye alifunga bao safi akipata pasi kutoka kwa Hamis Kiiza.
Hata hivyo, Simba walikuwa wanaweza kuibuka na ushindi mnono zaidi, lakini Ajib ambaye amekuwa mchezaji hatari, alikosa penalti katika dakika ya 83.

“Nilitegemea kupata ushindi mnono zaidi siyo huu wa bao 1-0, niliamini kuwa tunaweza kupata angalau ushindi wa mabao 6-0,” alisema Mayanja.Ushindi huu umewafanya Simba wafikishe pointi 42 wakiwa nyuma ya Yanga ambao walishinda jana dhidi ya JKT Ruvu yenye pointi 43 na hivyo kuendeleza kasi ya wakubwa hao ya kuwania ubingwa.

Hata hivyo, Kagera ambao msimu huu hawakuonyesha kiwango kizuri, walimaliza mchezo huo pungufu baada ya mchezaji wao Daudi Jumanne kupewa kadi nyekundu kutokana na kumkwatua Abdi Banda kipindi cha pili.

Bado Simba watabaki mkoani humo kwani mchezo wao unaofuata watakuwa hapohapo Shinyanga wakati watakapovaana na Stand wikiendi ijayo, kama watashinda mchezo huo watakuwa wamebakiza pointi tisa tu mkoani na kuwa na nafasi kubwa zaidi ya kutwaa ubingwa kwa kuwa wamekuwa na urahisi zaidi kushinda kwenye Uwanja wa Taifa.

Yanga wenyewe wanasafiri kwenda kwenye michuano ya kimataifa nchini Mauritius na hivyo watarejea hapa Simba wakiwa mbele yao kwa mchezo mmoja nap engine wakiwa juu yao katika msimamo watakapovaana Februari 20.

Leave A Reply