The House of Favourite Newspapers

TFF yamwondoa rasmi Yondani mechi ya Simba

0

Beki wa Yanga, Kelvin Yondani. 

BAADA ya Championi kuwa gazeti la kwanza kuripoti kuwa beki wa Yanga, Kelvin Yondani ataukosa mchezo dhidi ya Simba jana Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limethibitisha rasmi.
Championi toleo la Jumatatu namba 1762, lilikuwa na kichwa cha habari ‘Yondani atemwa mechi ya Simba’.

 
TFF jana Ijumaa imemwondoa rasmi Yondani katika mechi hiyo ya Ligi Kuu Bara dhidi ya Simba itakayochezwa Februari 20, mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Uamuzi huo umefikiwa baada ya Yondani kubainika alifanya kosa la kikanuni kinyume na kanuni ya 25 inayozungumzia udhibiti wa wachezaji kifungu cha kwanza.

 
Yondani alituhumiwa kumpiga daktari wa Coastal Union ya Tanga, Kitambi Maganga katika mchezo wa ligi hiyo kwenye Uwanja wa Mkwakwani, Tanga ambapo Yanga ilifungwa mabao 2-0.
Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi Tanzania (TPLB), Boniface Wambura aliliambia Championi Jumamosi kuwa, hatua hiyo ilifikiwa juzi Alhamisi baada ya Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi ya Bodi ya Ligi ‘Kamati ya Masaa 72’ kukutana na kupitia ripoti zote za ligi kuu na ile ya daraja la kwanza.
Kanuni ya 25 inasema; “Mchezaji atakaye

 
tolewa nje kwa kadi nyekundu kwa kosa la kupiga au kupigana atasimama kushiriki michezo mitatu (3) inayofuata ya klabu yake na atalipa faini ya Sh 500,000 (Sh laki tano) za Kitanzania.”
Tayari Yondani ameshakosa mechi mbili za ligi ambazo ni dhidi ya Prisons na JKT Ruvu, hivyo bado moja ambayo ni dhidi ya Simba.
“Baada ya kupitia ripoti hizo, ilibaini kuwa Yondani alifanya kosa hilo kwa kumpiga daktari wa Coastal Union kwa kutumia sanduku dogo la huduma ya kwanza jambo lililomfanya mwamuzi kumwonyesha kadi nyekundu.

 
“Kutokana na hali hiyo Yondani ataikosa michezo mitatu ya ligi kuu lakini pia atatakiwa kulipa faini ya shilingi 500,000, endapo atakuwa amemaliza kuitumikia adhabu yake,” alisema Wambura.
“Ripoti hiyo ilionyesha kuwa baada ya kipa wa Coastal Union kuumia, Yondani alifika kwa daktari huyo na kumuomba maji lakini alimnyima jambo ambalo lilimfanya Yondani achukue uwamuzi huo wa kumpiga.”

Leave A Reply