The House of Favourite Newspapers

Yanga fitna tupu… Ghana

0

 

 

IMG_8324

Mshambuliaji  wa Kimataifa wa Yanga, Donald Ngoma  (kushoto) akiwa na kocha wao.

 

Mwandishi Wetu, Accra

KIKOSI cha Yanga kiliondoka nchini juzi Jumamosi alfajiri kuelekea Ghana kikiwa na wachezaji 21 na viongozi tisa wakiongozwa na Mwenyekiti wa Chama cha Wachezaji wa Soka Tanzania (Sputanza), Musa Kisoki, kwa Ndege ya Shirika la Kenya Airways huku wakionekana ni wenye matumaini kibao.

Lakini inaonekana kama wenyeji wao Medeama SC ya Ghana wameweka fitna mbele baada ya kuipeleka mechi hiyo mbali kwenye uwanja mdogo wa Sekondi-Takoradi unaochukua watu 20,000, kwani Yanga walilazimika kusafiri hadi usiku na kufika wakiwa wamechoka sana.

IMG_8332

Kiungo wa Yanga, Haruna Niyonzima.

Yanga ilifika jijini Accra majira ya saa 12 jioni kwa saa za Ghana, Tanzania ikiwa ni saa tatu usiku na kulazimika kusafiri usiku huohuo hadi kufika kwenye mjini wa Tarkwa walikofika saa tano usiku kwa saa za huko ikiwa ni saa nane usiku kwa Tanzania. Walitumia basi lililoandaliwa na wenyeji wao ambalo lilitakiwa kusafiri usiku huohuo kuwapeleka wanapotaka kwenda.

Hofu nyingine ya hujuma ni kutokana na uwanja kuwa mbali na Accra hali ambayo inaonyesha ni kama ilivyotokea kwenye mchezo wa kufuzu hatua ya makundi dhidi ya Sagrada Esperanca ambapo Yanga walifanyiwa hujuma nyingi wakiwa kwenye uwanja mdogo wa timu hiyo.

Hali hii inaonyesha kuwa Uwanja wa Sekondi upo karibu na nyumbani kwa Medeama, kuna wasiwasi kwamba huenda mambo ya hujuma yanaweza kuhusika.

Yanga itacheza na Medeama katika mchezo wa Kombe la Shirikisho Afrika kesho Jumanne majira ya saa tisa kwa saa za Ghana huku Tanzania ikiwa ni saa 12:00 jioni.

IMG_8364

 

Lakini kama ilivyokuwa katika mchezo wa kwanza kwenye Uwanja wa Taifa, Dar baina ya timu hizo, waamuzi wa mechi hiyo walitoka kwenye nchi ya Kiarabu ya Misri na huku Ghana waamuzi wanatoka kwenye ukanda huohuo ambapo sasa wanatokea Morocco.

Hata hivyo, Yanga ambao wanaonekana kupambana na fitina za Waghana hao jana saa 12 jioni kwa saa za Tanzania walifanya mazoezi yao na kuonekana wachezaji wote wakiwa na morali ya hali ya juu.

Washambuliaji wawili wa timu hiyo, Mrundi Amissi Tambwe na Simon Msuva wamedai kuwa kesho watapambana kufa na kupona ili kuhakikisha Yanga inaibuka na ushindi katika mechi hiyo. Yanga inahitaji ushindi tu ili kufufua matumaini ya kutinga nusu fainali.

Wakizungumza na Championi Jumatatu wakiwa nchini Ghana, wachezaji hao wamedai kuwa mechi hiyo ndiyo fainali yao kwani wakipoteza basi huo ndiyo utakuwa mwisho wao wa kusonga mbele katika michuano hiyo.

“Tunamshukuru Mungu kwa kila kitu kwani tupo vizuri mpaka sasa lakini jambo kubwa ambalo linatuumiza vichwa ni mechi yetu ya Jumanne dhidi ya Medeama.

“Tangu tunatoka Dar es Salaam akili yangu yote inafikiria mechi hiyo, hakika sina cha kusema zaidi ya kuhakikisha siku hiyo tunaibuka na ushindi hata kama ni kufia uwanjani ni bora iwe hivyo,” alisema Msuva.

Kwa upande wake, Tambwe alisema: “Tuna kazi kubwa ya kufanya ili kufufua matumaini yetu ya kusonga mbele katika michuano hii, vinginevyo huo ndiyo utakuwa mwisho wetu.

“Binafsi namuomba Mungu anijalie uzima ili tuweze kuibuka na ushindi katika mchezo huo.”

 

Leave A Reply