The House of Favourite Newspapers

Anayekamatwa kwa Uchawi, Huliwa Nyama Yake, Kabila la Wala Watu-9

WAKATI ulaji wa nyama za watu ukitajwa kuwa hufanywa kutokana na matambiko maalum ya baadhi ya makabila nchini Papua New Guinea, kuna wengine wanasema ulaji upo kwa ajili ya dawa.

Wapo wanaopinga kutokana na ukweli kwamba kuna wakati Wazungu saba waliliwa kwa mpigo kama tutakavyoona katika matoleo yajayo ya makala haya kiasi cha kusababisha serikali kushtuka na kuanza kuwasaka waliofanya kitendo hicho kibaya.

Hakika ulaji wa nyama za watu siyo kwa ajili ya matambiko. Wakorowai ambao ndiyo kabila linaloongoza kwa kula nyama za watu nchini humo, vijana wao wanaochaguliwa kuingia katika kazi ya kuua, kukatakata nyama za watu na kuzipika, kwanza huchanjwa chale nyingi mwilini kwa kitu chenye ncha kali kisha kupakwa dawa. Vidonda hivyo vikipona huacha alama  ambazo watafiti waliokwenda kulitembelea kabila hilo walizipa jina la tattoo japokuwa hizo ni chale. Wakati wa kuchanja chale hizo, kijana hufungwa kwa kamba mikononi ili asiwe na uwezo wa kumzuia mchanjaji wakati akifanya kazi zake.

Mara baada ya kuchanjwa, hupakwa dawa ya kienyeji ambayo huzuia damu kutoka japo inasababisha maumivu makali kwa mtu aliyechanjwa. Baadaye mtu aliyechanjwa hupelekwa kwenye Mto Ndeiram Kabur  ambao hutumika sana kwa kusafiri kutoka vijiji vya kabila hilo hadi sehemu nyingine ya nchi.

Watafiti Waingereza waliokwenda kwenye makazi ya kabila hilo la Korowai wanasema siku ya kwanza kwenda kwenye vijiji hivyo walikwenda kwa kutumia mtumbwi kupitia mto huo.

“Tulipofika sehemu fulani tulishitukia tukivamiwa na watu waliokuwa uchi, mtu aliyekuwa akitutafsiria, Bwana Kembaren alisema watu hao walikuwa wanashangazwa na ngozi yetu,” alisema mtafiti mmoja.

“Nilimuona mtu mmoja, pande la mtu likiweka sawa mshale na upinde yule mtu aliyekuwa akitusindikiza (guard) akasema tuache kupiga makasia, tukatii, mtumbwi ukawa unaserereka.

“Hatukuwa na ujanja, walitoa amri ya sisi kushuka kwenye mtumbwi, kwa kweli tuliogopa sana kwani tulijua sasa ni zamu yetu ya kufanywa kitoweo na watu hao,” alisema mmoja wa watafiti hao.

“Hatuna nia ya kuwadhuru,” alisema mmoja wa wale watu, mfasiri wetu Kembaren aliwaambia kwamba tulikwenda huko kwa amani, hatukuwa na nia mbaya. Mmoja wa wale watu wakiwa watupu aliwasogelea lakini mkalimani wao, Kembaren alisisitiza kwa Wazungu hao kwamba watulie na wasiwe wamepaniki kwani kufanya fujo yoyote kutasababisha kifo kwao.

Baadaye Wazungu wote wakawa kama mateka na walipelekwa katika moja ya kijiji na ikatolewa maiti ya chifu wao aliyekaushwa kwa moto anayejulikana kwa jina la Moctezuma ili dua maalum ifanyike, hawakuelezwa dua hiyo ilikuwa kwa ajili ya nini lakini ilielezwa ikiwa mtu anauawa ili kuliwa,  nyama ya sehemu ya paja iliyokolezwa pilipili huwekwa karibu na maiti hiyo kibandani.

Kitendo cha maiti hiyo kutolewa nje kiliwatisha watafiti hao kwani waliwahi kusikia simulizi hiyo, hivyo wakajawa na hofu na wengi wakawa wanatokwa jasho la uoga wa kuliwa. Baadaye ngoma ilipigwa na wenyeji walijaa kuwashuhudia Wazungu hao, kiongozi wao alitumia nafasi hiyo kuwahutubia wananchi wake. Hata hivyo, mwandishi Mwingereza aliyeandika habari hii alisema hakuwa anaelewa kile alichokuwa akisema kiongozi yule wa kimila.

Kabila la Korowei lipo nyuma sana kimaendeleo na limetajwa kwamba ndilo lililohusika kumpika supu kijana Michael, mtoto wa aliyekuwa Makamu wa Rais wa Marekani, Nelson Rokeffeller  aliyepotea kiajabu na hakuonekana tena na baadaye kujulikana kwamba aliliwa.

Kabila hili lina taratibu moja, licha ya kula watu lakini kama mwanaume anakamatwa kwa kujihusisha na uchawi, adhabu yake naye huwa ni kuliwa nyama yake, kitendo hicho kwa lugha yao hukiita khakhua.

Comments are closed.