The House of Favourite Newspapers

Kwa Hili Basata Kweli Wanaonea Wasanii?

0
Snura Mushi.

Na BONIPHACE NGUMIJE| GAZETI LA IJUMAA| MAKALA

KUMEKUWA na malalamiko mengi kuhusu utendaji kazi wa Baraza la Sanaa Tanzania (Basata). Wasanii wamekuwa wakilalamikia baraza hilo huku wakihusisha baadhi ya uamuzi inayoutoa hasa wa kufungia kazi za wasanii na kudai wanafanya uonevu.

Mungereza: Watanzania wanatakiwa kuelewa kuwa Basata ni taasisi ya kiserikali. Kama taasisi ya kiserikali sheria inatutaka kuheshimu mamlaka. Kwa hiyo kiutendeji hatukuona tatizo

Ambwene Yesaya ‘Ay’.

Miongoni mwa wasanii ambao wamewahi kufunguka wazi juu ya Basata kuwaonea ni Emmanuel Elibariki ‘Nay wa Mitego’. Nay ambaye hivi karibuni baada ya wimbo wake wa Wapo kufungiwa na Basata kwa kile kilichodaiwa kuimba mashairi yenye uchochezi ndani yake na baada ya muda mfupi Rais Dkt. John Magufuli kuufungulia, alisema;

“Basata wanatakiwa kuelewa kuwa ninapokuwa natoa wimbo mashabiki wanakuwa na ‘atensheni’ ya kusikiliza nimeimba nini, sasa wanaposikia mijadala inaibuka kila mmoja akizungumza lake baada ya mimi kutoa wimbo, wao (Basata) huamua muda mwingine kufungia nyimbo zangu kutokana na maoni ya mashabiki jambo ambalo huwa siyo sawa.” Nay aliongeza pia kuwa baraza hilo limewahi kumuingizia hasara ya shilingi milioni 30 alizotumia kuandaa video ya Wimbo wa Pale Kati Patamu baada ya wao kuufungia, lakini pia dili la ubalozi ambalo alikuwa amesaini linalofi kia shilingi milioni 50.

Kutokana na malalamiko hayo ya Nay wa Mitego, wasanii wenzake na baadhi ya mashabiki mitandaoni, Ijumaa liliamua kumvaa katibu mkuu wake, Godfrey Mungereza na kufanya naye mahojiano, soma hapa chini; Ijumaa: Hebu wajuze Watanzania majukumu hasa ya Basata.

Nay wa Mitego.

Mungereza: Basata ni taasisi inayohusika na kukagua, kuboresha, kulinda utamaduni katika sanaa na kuhakikisha sanaa nchini inakua. Lakini mbali na hayo baraza linahusika pia kutoa elimu kwa wasanii wa nyanja mbalimbali juu ya sanaa na kufahamu wajibu wao kama wasanii, kufahamu haki zao na kulinda masilahi yao.

Ijumaa: Kwa mwaka mnakagua kazi ngapi za muziki?

Mungereza: Zaidi ya mia nane (800), hapa nazungumzia kwa Muziki wa Bongo Fleva tu, lakini bado kwenye Injili na kwingineko kwa hiyo tunakagua kazi nyingi.

Ijumaa: Mnapokagua mnatumia utaratibu gani kufungia kazi za wasanii hasa kwenye upande wa muziki?

Mungereza: Jambo la kwanza huwa tunaangalia maudhui ya nini msanii ameimba kwenye wimbo wake. Lakini pia kabla ya kufungia kazi ya msanii huwa tunatoa ushauri kwa msanii kwenda kufanya mabadiliko ya wimbo wake hasa pale tunapoona kuna ukiukwaji wa maadili. Hawa wengi unaoona tunafungia kazi zao huwa tumeshawaonya sana juu ya maudhui wanayoimba ama wametoa kazi isiyo na maadili bila kuipitisha barazani.

Shilole

Ijumaa: Kuna baadhi ya wasanii wamekuwa wakilalamikia juu ya kufungiwa nyimbo zao na kudai mnawaonea. Hili unalizungumziaje?

Mungereza: Kwa nini tumuonee msanii? Kwa faida ipi? Ninachokiona hapa kwenye suala hilo ni juu ya uelewa na mambo ya mihemko ya wasanii wakitaka kupata kiki kwa kazi ama nyimbo ambazo zinakiuka maadili. Wasanii wanatakiwa waelewe kuwa baraza linafanya kazi kwa weledi na linazingatia sheria.

Ijumaa: Kuhusu Nay wa Mitego kulalamika kumuonea kwa kuufungia wimbo wake wa Wapo kabla ya JPM kuufungulia, una lipi la kusema?

Mungereza: Si kweli kuwa tulimuonea. Kwanza Nay ni shahidi kuwa amekuwa akileta hapa nyimbo zake na kukaguliwa kabla hazijatoka na amekuwa akitupongeza. Sasa wimbo huu kwanza hakuuleta hapa, lakini kuhusu rais kuufungulia ni fursa kwa wasanii wengine kujifunza kuwa nyimbo zao zinafi ka mbali na viongozi wanapata nafasi ya kuzisikiliza.

Ijumaa: Hili la rais kutengua kifungo cha wimbo huo katika upande wa taswira yenu ya kiutendaji mnalizungumziaje?

Mungereza: Watanzania wanatakiwa kuelewa kuwa Basata ni taasisi ya kiserikali. Kama taasisi ya kiserikali sheria inatutaka kuheshimu mamlaka. Kwa hiyo kiutendeji hatukuona tatizo.

Ijumaa: Kwa upande wa muziki, ni wasanii gani ambao mara kwa mara mmekuwa mkiingia nao kwenye migogoro ya kimaadili?

Mungereza: Wapo wengi, kwa kuwa tumekuwa tukiwaita na kuwahoji na kuahidi kujirekebisha siwezi kuwaweka wazi hapa. Ijumaa: Kuhusu ‘mavideo queen’ wanaokwenda kinyume na maadili katika kazi zao huwa mnawashugulikia vipi?

Mungereza: Ikishakuwa video inakuwa si chini yetu tena. Hilo linawahusu Bodi ya Filamu na Michezo ya Kuigiza. Lakini tunafahamu wapo mavideo queen ambao pia ni wanamuziki na wanakiuka maadili ya Kitanzania hasa kwa picha zao mitandaoni. Tunawasikia na kuona hawa mabinti kina Gigy Money, Tunda, Shilole, Amber Lulu na wengine wengi wanaweka mitandaoni wakati mwingine picha ambazo si nzuri kimaadili.

Kuna sheria za mitandao zinaweza kupambana nao lakini pia wanatakiwa kufahamu wanachokifanya hakileti picha nzuri kwenye jamii.

KUMBUKA; AY na Snura ni kati ya wasanii ambao kwa nyakati tofauti waliwahi kuonja makali ya Basata.

Leave A Reply