The House of Favourite Newspapers

Kwa Takwimu Ajibu Vs Okwi Ni 100 Kwa 100

0
Ibrahim Ajibu wa Yanga.

WAKATI vikosi vya Simba na Yanga vikiwa kwenye maandalizi kabambe kwa ajili ya mechi ya Ngao ya Jamii, takwimu zinaonyesha washambuliaji wawili wa timu hizo, Ibrahim Ajibu wa Yanga na Emmanuel Okwi wa Simba wanaenda sambamba.

 

Ajibu alijiunga na Yanga hivi karibuni akitokea Simba kwa mkataba wa miaka miwili huku Okwi alisajiliwa na Simba akitokea kwao Uganda katika Klabu ya Sport Club Villa.

Emmanuel Okwi katikati.

Wachezaji hao mpaka sasa kila mmoja ameshaitumikia timu yake kwa dakika 270, ambazo ni sawa na mechi tatu, pia wote kila mmoja akifunga bao moja na kutoa pasi moja ya bao (yaani asisti). Ajibu ameshaitumikia Yanga kwenye mechi dhidi ya Singida United, Ruvu Shooting na Mlandege ya Zanzibar, ambapo kwenye mchezo huu alifunga bao moja na kutoa asisti kwa mchezaji mwenzake, Emmanuel Martin.

 

Mechi iliisha kwa Yanga kushinda mabao 2-0. Okwi yeye alianza kuonekana uwanjani mbele ya Bidvest Wits ya Afrika Kusini kisha akacheza mechi ya Simba Day dhidi ya Rayon Sports ya Rwanda ambapo alitoa pasi ya bao kwa Mohammed Ibrahim ‘Mo’.

 

Kisha Mganda huyo akaja kuibuka shujaa alipofunga bao pekee kwenye ushindi mbele ya Mtibwa Sugar kwenye mechi iliyopigwa Uwanja wa Taifa, Dar wikiendi iliyopita hivyo kulingana na Ajibu. Tayari mashabiki wa timu zote mbili wameshaanza tambo zao kuelekea mchezo wa Ngao ya Jamii, Jumatano ijayo huku kila upande ukiamini kuwa utaibuka na ushindi kwenye mchezo huo.

SAID ALLY, CHAMPIONI JUMATANI

Leave A Reply