MKUU wa benchi la ufundi la Yanga, George Lwandamina, raia wa Zambia, amefunguka kuwa ameandaa mikakati madhubuti ya kuhakikisha kikosi chake kinafanya vizuri na kuibuka na pointi sita kwenye michezo yao miwili ambayo wataicheza Kanda ya Ziwa dhidi ya Kagera Sugar ya Kagera na Stand United ya Shinyanga.
Yanga ambayo iliondoka jana Alhamisi kuelekea Kagera kwa ajili ya kucheza na Kagera Sugar kwenye muendelezo wa Ligi Kuu Bara, itashuka uwanjani kesho Jumamosi kwenye Uwanja wa Kaitaba, Kagera.
Baada ya hapo, Yanga itakuwa na kibarua kigumu dhidi ya Stand United kwenye mchezo wa ligi Oktoba 22, mwaka huu kwenye Uwanja wa Kambarage, Shinyanga. Mara ya mwisho uwanjani hapo Yanga walifungwa bao 1-0.
Akizungumza na Championi Ijumaa, Mzambia huyo alisema kuwa licha ya kutambua ugumu ambao upo mbele ya michezo hiyo lakini amejiandaa kupata pointi sita ambazo zitawapunguzia presha kabla ya kukutana na wapinzani wao Simba, Oktoba 28, mwaka huu.
“Najua ugumu uliopo mikoani ambapo mara nyingi timu haipati matokeo kirahisi kutokana na wapinzani kujiandaa kuzibakisha pointi zao na kutopata matokeo mabaya, lakini nikwambie kwamba tunaenda huko tukiwa na lengo moja pekee la kushinda.
“Nimepanga kupata pointi zote sita kwenye michezo miwili tutakayocheza huko mbele ya Kagera Sugar na Stand United, kwani tukipata pointi hizo itakuwa rahisi kwetu kupunguza presha ambayo tutakuwa nayo wakati tutakaoenda kukutana na wapinzani wetu Simba, kwenye mchezo wa tatu baada ya hii miwili,” alisema kocha huyo.