The House of Favourite Newspapers

Ujio wa Tshishimbi Noma

Kiungo mahiri wa Yanga, Papy Kabamba Tshishimbi.

KIUNGO mahiri wa Yanga, Papy Kabamba Tshishimbi leo atasimama kwenye kiungo cha juu kuhakikisha kwamba Ruvu Shooting haifurukuti kwenye mechi ya ligi kuu itakayopigwa kwenye Uwanja wa Taifa.

 

Tshishimbi katika mazoezi ya jana Jumamosi, alimfunga kipa Benno Kakolanya bonge la bao mithili ya lile la Shiza Kichuya wa Simba aliloifunga Yanga kwa kona msimu uliopita.

 

Mkongomani huyo aliikosa mechi dhidi ya Mwadui kwa kile kilichodaiwa kuwa gari lake liliharibika akakosa mazoezi ya mwisho kujiandaa na mchezo huo, makocha wakampiga chini.

 

Beki wa kulia wa Yanga, Hassan Kessy alisema amegundua kuwa ana uwezo wa kufunga tangu alipoifungia JKU kwenye Kombe la Mapinduzi.

 

“Tumejipanga vizuri na nina imani kuwa tutaibuka na ushindi ili tuweze kurudi katika mstari wa ubingwa.

“Lakini pia katika mechi hiyo ni lazima nitaifunga Ruvu kwani nina uwezo wa kufanya hivyo kama kuna mtu ambaye aniamini basi ataona,” alisema Kessy.

 

“Pamoja na kuifunga Ruvu Shooting pia nitafurahi sana nikiifunga Simba katika mzunguko wa pili baada ya kuikosa katika hatua ya nusu fainali ya Kombe la Mapinduzi,” aliongeza mchezaji huyo wa zamani wa Simba.

 

REKODI

Timu hizo zinakutana wakati Yanga ikiwa nafasi ya tano baada ya kujikusanyia pointi 22, huku Ruvu Shooting ikijikusanyia pointi 11 katika nafasi ya 15. Timu hizo zote mechi zao za mwisho hazikuwa na matokeo mazuri.

Yanga ina rekodi nzuri tangu mwaka 2010, katika ligi zimekutana mara 12 na kushinda mechi kumi, huku ikitoka sare mbili. Haijafugwa hata mechi moja.

Rekodi nyingine inayoingia nayo Yanga kwenye

mchezo huo wa leo ni kuifunga Ruvu Shooting mabao mengi zaidi ambayo ni 30, huku yenyewe ikifungwa manne pekee tangu mwaka 2010.

 

Katika msimu wa 2013/14, mchezo wa raundi ya kwanza, Yanga iliibuka na ushindi wa bao 1-0, ziliporudiana Yanga ikashinda mabao 7-0. Pia kwenye msimu uliofuata, mechi ya kwanza matokeo yalikuwa suluhu, ya pili Yanga ikashinda mabao 5-0. Mechi hizo zote zilichezwa kwenye Uwanja wa Taifa.

 

Ikumbukwe kuwa, msimu wa 2015/16, timu hizo hazikukutana kutokana na Ruvu Shooting kushuka daraja na kushiriki Ligi Daraja la Kwanza.

Massau bwire ambaye ni msemaji wa Ruvu Shooting amesisitiza kwamba rekodi haziwababaishi watapambana uwanjani.

 

AJIBU ALIVYONG’ANG’ANIWA NA MASHABIKI

Comments are closed.