The House of Favourite Newspapers

Pluijm Adai Pointi Za Mbao Za Moto

Kocha wa Singida United, Hans van Der Pluijm.

KOCHA wa Singida United, Hans van Der Pluijm, amesema pointi tatu walizopata dhidi ya Mbao FC zilikuwa za moto kwao kwani hawakuzipata kirahisi huku Simba, Yanga na Azam FC zikizikosa.

 

Jumatano wiki hii, Singida United iliifunga Mbao FC mabao 2-1 na kupata pointi tatu jambo ambalo halikuweza kufanywa na Simba, Yanga na Azam ambazo ziliambulia sare na timu hiyo.

 

Baada ya ushindi huo ilioupata kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza, Singida United sasa imefikisha pointi 33 na ipo katika nafasi ya nne kwenye msimamo wa Ligi Kuu Bara.

Yanga ilifungwa mabao 2-0 na Mbao FC huku Simba ikitoka sare ya mabao 2-2 na Azam ikatoka suluhu na timu hiyo.

 

Akizungumza na Championi Jumamosi, Pluijm raia wa Uholanzi alisema ulikuwa mchezo mgumu lakini walipambana na kupata ushindi tofauti na Simba na Yanga zilizobanwa.

 

“Ni furaha kupata matokeo katika uwanja wa wapinzani wetu sababu haikuwa rahisi, kama mnavyofahamu awali Yanga alipoteza hapa, Simba na Azam wakatoa sare lakini sisi tumeondoka na ushindi leo.

 

“Kwa matokeo haya, bado tunaendelea kujipanga kupambana kwani ligi imekuwa ngumu na ushindani unaongezeka na kwenye mzunguko huu hakuna timu iliyo tayari kufungwa,” alisema Pluijm.

Stori: Martha Mboma | Global Publishers

Comments are closed.