The House of Favourite Newspapers

Simba Imevuna Mkwanja Mrefu

WAKATI leo hii Simba ikitimiza miaka 82 tangu kuanzishwa kwake mwaka 1936, Championi Jumatano limefanya uchunguzi wake na kubaini kuwa, Simba ni kiboko ya Yanga kwa kujipatia fedha za kigeni kwa kuuza wach-ezaji nje ya nchi.

 

Tangu kuanza kwa karne hii ya 21, Simba imefanikiwa kuuza nje ya nchi zaidi ya wachezaji 11 tena kwa vitita vikubwa.

Kwa upande wa Yanga, wao wameonekana ni vinara wa kutoa wachezaji kwa majaribio kama si kuondoka bure.

 

Edibily Lunyamila, Bakari Malima, Jery Tegete, Dan Mrwanda, Mrisho Ngassa na wengine wengi wote wameonja raha  ya kimataifa wakitokea Yanga lakini si kwa kuuzwa.

 

Ifuatayo ni orodha ya wachezaji waliotoboa kimataifa kwa  Yanga na Simba, ingawa baadhi thamani zao hazikuweza kupatikana kutokana na ujanjaujanja wa viongozi wa klabu hizo.

Wachezaji waliouzwa kwa upande wa Yanga ni:

Shaban Nonda

Anatajwa kuwa mchezaji wa heshima kwa Yanga akiwa ni mchezaji pekee aliyepata mafanikio makubwa katika historia ya klabu hiyo.

 

Nonda ambaye ni raia wa DR Congo alijiunga na Yanga akitokea Atletico Olympic mwaka 1993, lakini mwaka 1994 Yanga ilimuuza kwa timu ya Vaal Professional ya Afrika Kusini kwa dola 10,000 (zaidi ya Sh milioni 20 kwa kiwango cha sasa).

 

Mbali na timu hizo, pia Nonda alizitumikia timu kubwa barani Ulaya zikiwemo Blackburn Rovers ya England na Monaco ya Ufaransa.

 

Said Maulid ‘SMG’

Mwaka 2008, Yanga ilimuuza nyota huyo kwa  Klabu ya Onze Bravos Dos Marquis ya Angola baada ya kuvutiwa na kiwango chake. Waangola hao waliipatia Yanga kitita cha dola 50,000 (zaidi ya milioni 100 kwa sasa)

 

Nadir Haroub ‘Cannavaro’ 

Mwaka 2009 alipata dili nje ya nchi, baada ya kutolewa kwa mkopo wa malipo ya dola 3,000 (zaidi ya Sh 6,000,000 kwa sasa) katika timu ya Vancouver White Caps ya Canada. Hata hivyo hakudumu sana, kwani baada ya muda mfupi alirejea Bongo.

 

Simoni Msuva

Huyu ndiye mchezaji wa mwisho wa Yanga kuuzwa nje ya nchi, aliuzwa kwa Klabu ya Difaa Al Jadida ya nchini Morocco kwa dola 150,000 ( zaidi ya Sh milioni 350).

 

Upande wa Simba idadi ya waliotoboa ni kubwa.

 

Nteze John ‘Rungu’

Straika huyu mzaliwa wa Kigoma baada ya kuonyesha makeke akiwa na kikosi hicho kwenye michuano ya kitaifa na kimataifa, alifanikiwa kupata dili na kujiunga na timu ya Qwaqwa ya Afrika Kusini ambayo ni Free States kwa sasa, dau lake lilikuwa siri.

 

Mohamed Mwameja

Katika miaka ya 1990, Simba walikubali kumwachia na kwenda kujiunga na timu ya Jomo Cosmos ya Afrika Kusini.

 

Hata hivyo akiwa Afrika Kusini, Mwameja alifanikiwa kuuzwa Reading iliyokuwa inashiriki Ligi Kuu England, lakini alikosa kibali cha kufanya kazi nchini humo baada ya uongozi wa Reading kuomba uthibitisho kama kweli ni Mtanzania, hakucheza.

 

Selemani Matola 

Matola ambaye kwa sasa ni Kocha Mkuu wa Lipuli FC, aliuzwa kwenda Klabu ya Super Sport ya Afrika Kusini kwa kitita cha dola 20,000 (zaidi ya Sh milioni 40 kiwango cha sasa).

 

Patrick Ochan

Kiungo huyu raia wa Uganda alikuwa mhimili mzuri katika kikosi cha Simba katika miaka nane iliyopita lakini uongozi wa klabu hiyo uliamua kumuuza kwa timu ya TP Mazembe ya DR Congo kwa kitita cha dola 50,000 (Sh Milioni 130 viwango vya sasa).

 

Haruna Moshi ‘Boban’

Nyota huyu anaichezea African Lyon kwa sasa, Simba iliwahi kumuuza barani Ulaya kwa timu ya Gifle IF ya Sweden kwa dau la dola 50,000 ( Sh milioni 130 kwa sasa).

 

Mbwana Samatta

Simba ilimuuza kwa TP Mazembe kwa kitita cha dola 100,000 (zaidi ya Sh milioni 260 kwa sasa).

 

Emmanuel Okwi

Simba pia iliwahi kuumuza Okwi kwa Klabu ya Etoile du Sahel ya Tunisia kwa dola laki tatu (300,000) (zaidi ya Sh milioni 680 kwa sasa).

 

Mwinyi Kazimoto

Aliuzwa Al Markhya ya Qatar kwa kitita cha dola 50,000 (zaidi ya Sh milioni 130 kwa sasa).

 

Shomari Kapombe

Aliuzwa AS Cannes ya Ufaransa kwa Euro 30,000,  zaidi ya Sh milioni 75 kwa sasa).

 

Moses Odhiambo

Alitua APR ya Rwanda kwa dola 50,000 (za Sh 130 kwa sasa),

 

Victor Costa

Alienda Meritzburg United ya Afrika Kusini. Dau halikutajwa

 

Henry Joseph

Alisajiliwa na Kongsvinger ya Norway. Naye dau halikutajwa.

Angalizo: Orodha hii haijumuishi wachezaji waliokwenda kwa ajili ya kufanya majaribio, bali waliofanikiwa kuingia mikataba ya timu za nje.

Comments are closed.