WAFANYAKAZI wa Benki ya NMB jana walijitokeza kufanya usafi pamoja na jamii maeneo mbalimbali hapa nchini na kutoa msaada wa vitu kwa wahitaji na vifaa vya kufanyia usafi katika baadhi ya maeneo ikiwemo soko la feri.
Kwa jijini Dar es Salaam wafanyakazi hao wakiongozwa na viongozi waandamizi wa benki hiyo walifanya usafi eneo la Coco Beach pamoja na Soko la Samaki la Feri kwa kushirikiana na wananchi waliojitokeza kufanya usafi kwenye maadhimisho ya usafi duniani.
Hata hivyo mbali na kufanya usafi katika Soko la Feri walitoa msaada wa vifaa vya kufanyia usafi katika soko hilo, ikiwa ni kuhamasisha usafi kwa jamii na kuunga mkono shughuli hizo ambazo ni muhimu kwa jamii yoyote.
Akikabidhi vifaa vya kufanyia usafi Soko la Feri, Meneja wa Benki ya NMB Kanda ya Dar es Salaam na Zanzibar, Badru Idd alisema huo ni utaratibu wa kawaida wa benki hiyo kujitolea ama msaada au kushiriki moja kwa moja katika shughuli za kijamii ili kujenga ushirikiano kwa jamii wanayoihudumia.
Alisema Soko la Feri linahudumia watu mbalimbali ambao ni wateja wa Benki hiyo hivyo wana kila sababu kusaidia kuboresha huduma katika soko hilo. Vifaa alivyokabidhi kwa uongozi wa Soko hilo mara baada ya kuwasili ni pamoja na mifagio, reki, makoleo, mifuko maalum ya kuhifadhia na kuzolea taka na vifaa vya kujikinga wakati wa kufanya usafi.
Wakati zoezi hilo likifanyika Dar es Salaam na mikoa mbalimbali pia wafanyakazi wa Benki hiyo walifanya usafi maeneo mbalimbali pamoja na kutoa misaada kwa wahitaji hasa wagonjwa hospitalini.
Mkoani Dodoma wafanyakazi wa benki hiyo mbali na kufanya usafi walitembelea wodi ya akinamama Kituo cha Afya cha Makole na kutoa misaada mbalimbali kwa wagonjwa kituoni hapo. Mkoani Mbeya wafanyakazi walifanya usafi katika vituo vya mabasi pamoja na eneo la Kasumulo mpaka wa Tanzania na Malawi.
Comments are closed.