The House of Favourite Newspapers

Mkude, Kapombe Wamvuruga Mbelgiji

Kocha Mbelgiji Patrick Aussems.

KUTOKANA na muingiliano wa kimajukumu kwa wachezaji wa Simba ambao wameitwa Taifa Stars, kumemfanya Kocha Mbelgiji Patrick Aussems ashindwe kuwanoa baadhi ya wachezaji wake.

 

Stars kwa sasa ipo kambini ikijiandaa na mchezo wa kuwania kufuzu Kombe la Afrika dhidi ya Cape Verde na wachezaji wa Simba ambao wapo kikosini humo, ni Jonas Mkude, Shomari Kapombe, Aishi Manula na John Bocco.

Simba ambayo katika mchezo uliopita ilitoka suluhu dhidi ya Yanga, leo Jumamosi wataivaa Afri­can Lyon kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar saa moja usiku.

 

Awali, Shirikisho la Soka Tan­zania (TFF) lilikubaliana kuwa ligi haitosimama na badala yake   wachezaji wangeungana na klabu husika siku moja kabla ya mechi.

 Kwa upande wa Simba, wachezaji wao walitakiwa kuripoti kambini juzi Alhamisi jioni ili wakaungane na wenzao, lakini haikuwa hivyo na jana Ijumaa walifanya mazoezi asubuhi na Stars jambo ambalo halikuwafurahisha Simba kutokana na makubaliano kukiukwa.

 

Aussems alisema awali alikuwa ameandaa program na wachezaji wake wote lakini ilishindikana kuto­kana na baadhi yao ambao wapo kikosi cha kwanza kuwa na maju­kumu mengine timu ya taifa.

Kocha huyo alisema suala hilo lilivuruga mipango yake lakini hata hivyo ataiongoza timu hiyo kupata matokeo.

 

“Wachezaji wako vizuri kwa ajili ya kupambana, na mchezo huu tu­nahitaji ushindi na siyo kitu kingine, tumerekebisha yale makosa am­bayo tulionyesha kwenye mchezo dhidi ya Yanga.

“Tunawaheshimu wapinzani wetu lakini pia tunahitaji ushindi na ka­tika program zangu nimewakosa baadhi ya wachezaji ambao wapo timu ya Taifa.ingawa niliambiwa watarudi kabla ya mechi, hilo nalo limevuruga mipango yangu kwa kiasi lakini tutapambana kupata matokeo,” al­isema Mbelgiji.

 

Championi Jumamosi lilimtafuta Ofisa Habari wa TFF, Clifford Ndimbo azungumzie ishu hiyo ambapo alisema: “Kwa sababu wachezaji walikuwa kambi moja tukawataka wafanye ma­zoezi kwanza na Stars na baadaye wajiunge na klabu yao.”

 

Timu hizo zimeweka kambi sehemu moja katika Hoteli ya Sea Scape iliyopo Mbezi Beach jijini Dar.

MBELGIJI AWAZUIA OKWI, KAGERE

Wakati huohuo, Mratibu wa Simba, Abbas Ally ameweka wazi kuwa Aussems amewazuia nyota wake wa kimataifa walioitwa timu za taifa.

“Hadi sasa hakuna hata mchezaji wetu wa kimataifa aliyeondoka, kutokana na kupata taarifa mapema juu ya uwepo wa mchezo wetu wa kesho dhidi ya African Lyon.

 

“Kweli baada ya mchezo wetu wa Jumapili dhidi ya Yanga, kocha aliahidi kuwaruhusu waende kutumikia timu zao za taifa kwani alitegemea ligi ingesimama kupitisha kambi ya timu ya taifa, Taifa Stars, lakini baadaye aliwazuia baada ya kutan­gazwa kutosimama kwa ligi hivyo akawataka wabaki hadi wamalize mechi ya kesho (leo),” alisema Abbas

 

Wachezaji wanaotakiwa kujiunga na timu zao za taifa ni Meddie Kagere na Haruna Niyonzima wote raia wa Rwanda, Juuko Murshid na Emmanuel Okwi wote Uganda huku Clatous Chama akiitwa Zambia.

Comments are closed.