The House of Favourite Newspapers

Kakolanya Amponza Kigogo Yanga

Beno Kakolanya

MAMBO ni moto ndani ya Yanga. Hivyo ndivyo u n a v y o w e z a kusema baada ya kigogo mmoja wa klabu hiyo kukumbana na balaa kutoka kwa kocha mkuu wa timu hiyo, Mkongomani, Mwinyi Zahera.

 

Unajua ilikuwaje? Baada ya kipa wa timu hiyo, Ramadhani Kabwili kuumia katika mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya African Lyon ulichezwa Alhamisi iliyopita, huko jijini Arusha kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, kigogo huyo alimpigia simu Zahera ambaye yupo nchini Ufaransa na kumfahamisha juu ya tukio hilo kisha  kumuomba amsamehe Beno Kakolanya ili aweze kurudi kundini na kuendelea kuitumikia timu hiyo.

 

Ikumbukwe kuwa hivi karibuni Zahera alisema kuwa hataki kufanya kazi na Kakolanya katika kikosi cha Yanga kutokana na kitendo chake cha kugoma kuitumikia timu hiyo mpaka alipwe madai yake ambayo anaidai klabu hiyo jambo ambalo lilimkera vilivyo kocha huyo na kumuona kama msaliti kwa sababu si yeye pekee aliyekuwa anadai, hata wachezaji wenzake wengi klabuni wanadai lakini hawakugoma na wanaendelea kuitumikia timu hiyo kama kawaida.

Akizungumza na Championi Jumatatu kwa njia ya Simu, Zahera alisema kuwa baada ya kupigiwa simu na kigogo hiyo ambaye hakutaka kumtaja jina lake, alimwambia kuwa akamtafutie Kakolanya timu nyingine ya kucheza na siyo Yanga. “Nilishangaa sana kusikia kiongozi huyo ananiambia maneno hayo, kwani kabla sijaja huku niliwaambia kabisa kuwa sitaki kufanya kazi na msaliti, kama wanaona kuwa Kakolanya ni bora zaidi ya wachezaji wengine basi niwaachie timu yao.

 

“Nilimwambia kama anataka niendelee kuifundisha Yanga amtafutie timu nyingine, kwani kama Kabwili kaumia basi Kindoki (Klaus Kindoki) yupo atadaka na atakuwa akisaidiana na kipa wa timu ya vijana ila siyo Kakolanya kurudi kikosini kwani najua atanivurugia timu yangu.

 

“Nakumbuka siku ambayo Kakolanya alipewa hela na watu ambao wanadaiwa kujitolea kumlipa madai yake hayo, kuna baadhi ya wachezaji walinifuata na kuniambia kuwa kwa nini Kakolanya amelipwa na sisi hatujalipwa, kwani yeye ni bora kuliko sisi? Jambo hilo liliniumiza sana, kwa hiyo kama wanamhitaji wamtafutie timu akacheze ila siyo katika kikosi changu,” alisema Zahera. Katika hatua nyingine, Zahera amewatoa hofu mashabiki wa Yanga kwa kuwaambia: “Mimi bado ni kocha Yanga, hivyo nitarudi kuendelea na majukumu yangu Desemba 26, kwa hiyo wasiwe na wasiwasi.”

STORI NA SWEETBERT LUKONGE

Comments are closed.