The House of Favourite Newspapers

Maskini Ruge na Dimpoz!

Mkurugenzi wa vipindi wa Clouds Media, Ruge Mutahaba.

KUNA wengine hesabu za kuuingia mwaka mpya 2019, zimekuja na majibu mabaya, watakaoufikia salama, heri kumshukuru Mungu. Ukisikia kauli ya “maskini” ikiwaendea Ruge Mutahaba, Omary Faraji ‘Ommy Dimpoz’ na Rose Muhando ujue kuna jambo la huruma unatakiwa kulifanya juu yao.

 

Kwa muda mrefu watu hao maarufu nchini wamekuwa wakipigania afya zao katika hospitali mbalimbali kiasi cha kuwafanya ndugu na rafiki kutumia muda mwingi kuwaombea wapone haraka. Miongoni mwa watu waliofanya ibada maalumu ya kuwaombea Ruge na Rose waweze kupona haraka ni Mchungaji wa Mitume na Manabii, Daud Mashimo.

 

 

 

 

Huruma ya mtumishi huyo wa Mungu imekuja juu ya watu hao kutokana na kuwa wagonjwa kwa muda mrefu ambapo Ruge mara kadhaa ameripotiwa kutibiwa nchini Afrika Kusini akidaiwa kuwa na matatizo ya figo. Aidha, Rose yuko nchini Kenya akisumbuliwa na ugonjwa ambao haujafahamika, huku Dimpoz akielezwa kufanyiwa upasuaji wa koo kwa mara ya pili nchini Ujerumani na kisha kurejeshwa hospitalini Kenya kufanyiwa uangalizi wa kitabibu.

Rose Muhando

“Tumefanya maombi maalumu ya mkesha Desemba 28, mwaka huu kuwaombea Ruge na Rose, Bwana awafungue kutoka katika kifungo cha magonjwa yanayowatesa na ninaamini watasimama tena,” alisema Mchungaji Mashimo. Hata hivyo, uchunguzi unaonesha kuwa mitandao mingi na vyombo vya habari vinaporipoti kuhusu hali tete za kiafya za watu hao maarufu wengi wamekuwa wakihimiza jamii nzima kuendelea kuwaombea afya kwa Mungu.

 

Hivi karibuni gazeti hili liliripoti juu ya Dimpoz kurejea kutoka Ujerumani na kufanyiwa kliniki nchini Kenya, wengi kati ya waliosoma habari hiyo walionesha wamemmisi msanii huyo.

 

“Yaani sitaki kuamini kama tunafunga mwaka bila ya shoo ya Dimpoz, eee Mungu mponye mja wako,” ilisomeka komenti iliyowekwa kwenye akaunti ya Facebook ya Gazeti la Ijumaa Wikienda iliyoandika juu ya ugonjwa wa msanii huyo.

 

Wakati hali ya watu kummisi Ruge ilionekana wazi baada ya mdau huyo wa muziki ambaye pia ni Mkurugenzi wa Vipindi wa Clouds Media Group, kutoonekana katika Tamasha ya Fiesta lililofanyika wikiendi iliyopita katika Viwanja vya Posta jijini Dar. Kutokana na ukweli huo, Mkuu wa Mkoa wa Dar, Paul Makonda aliyekuwa mgeni rasmi katika tamasha hilo alilazimika kufanya sala maalumu ya kumuombea Ruge.

STORI: Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Comments are closed.