The House of Favourite Newspapers

Ajibu Auwasha Moto Yanga SC

Ibrahim Ajibu.

NAHODHA wa Yanga, Ibrahim Ajibu, amewataka wapenzi na mashabiki wa timu hiyo, kutokata tamaa kutokana na matokeo mabovu waliyopata kwenye mechi tatu zilizopita kwani wamepata dawa.

 

Yanga ambayo ilicheza michezo 19 bila kufungwa, ilijikuta ikipokea kichapo cha kwanza mbele ya Stand United kule Shinyanga kwa bao 1-0 baada ya hapo ikatoka suluhu mechi mbili mfululizo dhidi ya Coastal Union kule Tanga na Singida United ya mkoani Singida.

 

Kutokana na matokeo hayo, mashabiki na wadau wa timu hiyo walianza kuingiwa na hofu ya kukutwa na watani zao Simba ambao kama watashinda viporo vyote saba, watafikisha pointi 57 ikiwa pointi mbili zaidi ya Yanga wenye alama 55 baada ya kucheza mechi 22.

 

Kesho Jumapili Yanga itakuwa ugenini tena kuvaana na JKT Tanzania kwenye uwanja wa Mkwakwani, Tanga ambapo katika mchezo wao uliopita Yanga ilishinda 3-0, baada ya hapo itavaana na Simba Jumamosi ijayo.

 

Ajibu ameliambia Championi Jumamosi kuwa: “Kazi ndiyo kwanza imeanza, kwa hiyo Wanayanga wote tunawaomba waendelee kutuunga mkono, sare hizi mbili tulizopata zisiwavunje nguvu.

 

“Hata sisi wachezaji matokeo hayo hayajatufurahisha, ndiyo hivyo ishatokea lakini bado hatujakata tamaa, tutaendelea kupambana vilivyo katika mechi zote zilizobaki ili kuhakikisha tunapata ushindi.”

Stori na Sweetbert Lukonge, Championi Jumamosi

Comments are closed.