The House of Favourite Newspapers

Simba Pambaneni, Watanzania Tunasubiri Historia

WIKIENDI hii gumzo nchini ni mechi ya michuano inayoandaliwa na Ligi ya Mabingwa Afrika na Kombe la Shirikisho kati ya wenyeji Simba dhidi ya AS Vita.

 

Leo Jumamosi kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Simba itakuwa na shughuli pevu pale itakapokuwa ikisaka ushindi wa lazima kabisa ili iweze kutinga robo fainali ya michuano hiyo mbele ya Vita ya DR Congo saa 1 Usiku.

Simba ipo mkiani kwenye kundi lao ambalo ni D ikiwa na pointi sita hivyo itahitaji ushindi wa lazima ili kufikisha alama tisa ambazo zitawapeleka moja kwa moja robo fainali. Vinara wa kundi ni JS Saoura ya Algeria wenye pointi nane, Al Ahly ya Misri inafuatia ikiwa nazo saba sawa na Vita.

 

Kimahesabu Simba imekaa nafasi nzuri zaidi kwani yenyewe ikishinda haisubiri matokeo ya mechi kati ya Al Ahly dhidi ya JS Saoura ambayo nayo inapigwa leo saa 1 usiku kule Misri. Kama mechi yao itaisha sare basi Saoura na Simba ikashinda basi zitaenda robo fainali.

 

Kama Watanzania, tunapaswa kuungana kuishangilia na kuipa msaada utakaowasaidia Simba kupata kushinda na kusonga mbele zaidi huku ikipeperusha bendera ya Tanzania kimataifa. Jukumu letu kwa sasa ni kutanguliza utaifa mbele ili kuisaidia timu hii ya Tanzania kusonga mbele na kuifanya nchi yetu itoke kimasomaso katika medani ya soka Afrika.

Bodi ya Uhariri/ Maoni

Comments are closed.