The House of Favourite Newspapers

Tambwe Afunguka Kulogwa na Ngoma

MSHAMBULIAJI wa Yanga, Mrundi, Amissi Tambwe ndiye mchezaji anayetajwa kuwa bingwa wa kufunga mabao ya vichwa katika Ligi Kuu Bara.

 

Hali hiyo ni kutokana na umahiri wake mkubwa wa kuzifumania nyavu. Tangu atue hapa nchini msimu wa 2013/14 na kujiunga na Simba akitokea Vital’O ya Burundi na baadae Yanga, ndiye mcheza wa kulipwa anayeongoza kwa kufunga mabao mengi kuliko wote wanaoshiriki ligi kuu mpaka sasa.

Amissi Tambwe.

Tangu msimu huo wa 2013/14 mpaka sasa, Tambwe amepachika wavuni mabao 72 katika michuano ya ligi kuu pekee. Akiwa Simba alizifumania nyavu mara 20 ambapo, msimu 2013/14 alifunga mabao 19 na kufanikiwa kuibuka mfungaji bora lakini pia msimu wa 14/15 kabla ya kutua Yanga aliifungia timu hiyo bao moja. Msimu huo wa 2014/15 katika dirisha dogo la usajili alijiunga na Yanga na akaifungia timu hiyo mabao 13.

Kutokana hali hiyo alimaliza msimu huo akiwa amefunga jumla ya mabao 14 na kushika nafasi ya pili kwa kuzifumania nyavu katika michuano hiyo akiwa nyuma ya Simon Msuva aliyeibuka mfungaji bora msimu huo kwa kufunga mabao 17.

 

Msimu uliofuata, Tambwe aliibuka mfungaji bora wa ligi hiyo baada ya kuifungia timu hiyo mabao 21 jambo ambalo lilimwezesha kuvunja rekodi mbalimbali za wafumania nyavu wengine waliotangulia waliokuwa wakishikilia rekodi hiyo. Msimu 2016/17 licha ya kukabiliwa na changamoto ya kuumia mara kwa mara lakini alifanikiwa kuifungia timu yake hiyo mabao 12.

 

Hata hivyo, msimu wa 2017/18 ulikuwa ni mgumu kwa kwake aliumaliza bila kufunga bao lolote lile. Hali hiyo ilisababishwa na kuwa nje ya uwanja kwa muda mrefu kutokana na kusumbuliwa na maumivu ya goti lake la kushoto. Msimu huo aliwezakuitumikia Yanga katika mchezo mmoja tu wa ligi kuu ambao ulikuwa ni dhidi ya Mbao FC ya jijini Mwanza.

 

Lakini msimu huu wa 2018/19 ambao unafikia tamati hivi karibuni amefanikiwa kufunga mabao nane tu mpaka sasa na kumfanya afikiesha jumla ya mabao 72 katika michuano ya ligi kuu tangu atua hapa nchini.

 

Katika mahojiano maalumu na Spoti Xtra, Tambwe anasema kuwa changamoto ya kuumia msimu uliopita ndiyo iliyompotezea makali yake jambo ambalo linamfanya leo hii aonekane kuwa ni mchezaji wa kawaida tu.

 

ANAZUNGUMZIAJI HALI HIYO

“Bado roho yangu inaniuma kutokana na mabalaa niliyoyapitia msimu uliopita ambapo nilitumia muda mwingi nikiwa nje ya uwanja. “Nilikumbana na maumivu mengi, achana na maumivu ya goti lakini pia maumivu ya kukaa nje ya uwanja kwa muda mrefu bila kucheza.

 

“Pia nilikuwa naumia zaidi kila nilipokuwa nikiona matokeo mabaya ambayo timu yangu ilikuwa ikiyapata. “Kuna wakati nilikuwa nalazimisha kucheza ili tu niweze kuisaidia lakini hakuwezekana kwani kila nilipokuwa nikiingia uwanjani niliishia kuumia. “Kusema kwema nilipitia changamoto kubwa katika maisha yangu ya soka, kwamwe sitoisahau kabisa.

 

KWANI MSIMU HUU HAJAFANYA VIZURI?

“Nimemwomba sana Mungu
msimu huu hali hiyo ya kumia isitokee na ninamshukuru kwani mpaka sasa sijapata majeraha ya kuniweka nje ya uwanja kwa muda mrefu. “Nilitamani sana niandike rekodi nyingine msimu huu lakini imeshindikana kutokana na kutopata nafasi ya kucheza mara kwa mara. “Ila kama ningekuwa napata nafasi ya kucheza naamini nisinge kuwa na mabao hayo nane tu pengine na mimi ningekuwa nashindana na wanao-ngoza kwa sasa kwa kufunga mabao mengi,” anasema Tambwe.

 

JE, ALILOGWA KWELI?

“Kuna baadhi ya watu walikuwa wakiniambia kuwa nimelogwa na Donald Ngoma ili nishindwe kucheza soka lakini binafsi sikutaka kuyasikiliza mambo yao kwa sababu katika maisha yangu siku zote namwamini Mungu. “Ndiyo maana tangu nilipoumia siku zote nilikuwa nikihudhuria matibabu ya hospitali na siyo sehemu nyingine mpaka nilipopona, kwa hiyo sikuwa nimelogwa bali niliumia tu kama ambavyo wachezaji wengine huumia na kukaa nje ya uwanja kwa muda mrefu.

 

MIKAKATI YAKE

“Mikakati yangu ni kuendelea kuitumikia Yanga, kama wataamua kuniongezea mkataba. “Kama hawataniongozea basi nitajua nini cha kufanya ila kwa sasa bado napenda kuendelea kuitumikia Yanga.

 

KUHUSU KIKOSI CHA YANGA MSIMU HUU

“Hatukuwa na kikosi kibaya ila bahati haikuwa upande wetu, tunafanya vizuri tu katika mechi zetu nyingi na tukapoteza umakini katika mechi chache na zaidi ni zile mbili tulizocheza dhidi ya Ndanda FC pamoja na moja ya Mtibwa Sugar kule Morogoro. “Kama ni marekebisho kwa ajili ya msimu ujao ni nafasi chache tu ambazo kocha anapaswa kuzifanyia kazi ila kikosi chetu ni kizuri.

 

KUHUSU UONGOZI MPYA

“Viongozi ni wazuri kutokana na CV zao ambazo nimebahatika kuzisoma, kikubwa wanatakiwa kupewa ushirikiano tu naamini wataitoa timu hapa ilipo sasa na kuipeleka sehemu nyingine ambayo ni nzuri zaidi.

ANAMZUNGUZIAJE MWINYI ZAHERA

“Ni kocha mzuri mwenye mipango mingi, hakika amefanya kazi kubwa sana ambayo imewashangaza wengi licha ya changamoto nyingi ambazo tumepitia.

 

ANAIZUNGUZIAJE SIMBA

“Wana timu nzuri lakini na sisi pia tuna timu nzuri ndiyo manaa mpaka sasa bado tunachuana nao katika kuwania ubingwa. “Kama kuna vitu walituzidi basi ni vichache sana ambavyo ni vya nje ya uwanja, lakini vya ndani ya uwanja ni vichache ndiyo maana hata ukiangali msimao wa ligi sisi mpaka sasa tumefungwa mabao 24 na wao 21,” anasema.

STORI: SWEETBERT LUKONGE

Comments are closed.