The House of Favourite Newspapers

Ahukumiwa Jela Miaka 99 Kwa Makosa 17

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu imemhukumu kifungo cha miaka 99 jela Salma Mntambo baada ya kupatikana na hatia katika mashtaka 17 likiwemo la kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu.

 

Miaka hiyo 99 inatokana na makosa 14 ya kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu ambapo kwa kila kosa amehukumiwa miaka sita jela, huku katika makosa matatu ya kutoa nyaraka za uongo kila kosa amehukumiwa miaka mitano jela.

 

Hukumu hiyo imesomwa jana Septemba 18, 2019,  na Hakimu Mfawidhi Kelvin Mhina wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Akisoma hukumu hiyo, Hakimu Mhina,  alisema kwka mahakama kupitia mashahidi watano walioletwa na upande wa mashtaka,  wameweza kuthibitisha pasipo kuacha shaka kuwa mshtakiwa ametenda kosa hilo.

Hata hivyo,  Hakimu Mhina amesema adhabu hizo zitaenda pamoja,  hivyo mshtakiwa atakaa gerezani kwa miaka sita tu.

 

Pia mahakama imesema kuhusu suala la fidia atatafakari na kufanya utafiti ili aje kutoa oda ambayo ni sahihi,  hivyo Oktoba 2, mwaka huu,  atatoa oda hiyo ya fidia.

 

Katika kesi hiyo, mshtakiwa huyo alikuwa akikabiliwa na mashtaka 24,  hata hivyo,  ametiwa hatiani katika mashtaka 17 yakiwamo ya kutakatisha fedha ya jumla ya Sh. 1.027,000,000 kutoka kwa Ridhuan Mringo huku akijua fedha hizo zimetokana na zao la makosa tangulizi ya kugushi, kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu na kuwasilisha nyaraka za uongo.

 

Katika kosa la kugushi, mshtakiwa Mntambo anadaiwa kati ya June mosi 2003 na Oktoba 31, mwaka 2011,  maeneo yasiyojulikana wilayani Ilala, mkoani Dar es Salaam,  kwa nia ya udanganyifu alighushi risiti yenye namba 001226 ya tarehe 10/06/2003 ili kuonyesha kwamba Ridhuan Mringo alinunua nyumba ya Shirika la Nyumba iliyopo Plot namba 710 mtaa wa Mfaume Upanga kwa Sh. Millioni 70 wakati akijua ni uongo.

Comments are closed.