The House of Favourite Newspapers

Bocco Sasa Atua Mlangoni Simba SC

WAKATI timu pinzani kwa Simba zikiwa zinapata taabu ya kumzuia straika Meddie Kagere kwenye mechi za Ligi Kuu Bara, taarifa kutoka kwenye benchi la ufundi la Simba ni kuwa safu yao ya ushambuliaji itazidi kuwa moto kutokana na straika na nahodha wao John Bocco kurejea kuichezea timu hiyo.

 

Nahodha huyo wa Simba hadi sasa bado hajaichezea timu yake mechi yoyote tangu mwezi Agosti kutokana na kuwa nje baada ya kupata majeraha.

 

Bocco amekosa mechi ya Ligi ya Mabingwa Simba ikicheza na UD do Songo sambamba na mechi nne za Ligi Kuu Bara. Akizungumza na Championi Jumatano, Meneja wa Simba, Patrick Rweyemamu amethibitisha juu ya kurejea kwa straika huyo ambaye atarejea na kuungana na wenzake hivi karibuni baada ya sasa kuwa fiti kufuatia kuwa nje.

“Bocco amerejea na ataonekana hivi karibuni akiwa na wenzake ikiwa ni baada ya kuwa nje kwa miezi kadhaa kutokana na kupata majeraha ambayo yamemfanya akose mechi zetu za ligi na michuano ya kimataifa.

 

“Ameshapona na ataanza mazoezi mepesi ili arejeshe fitinesi na baadaye ataanza kucheza kwenye ligi baada ya kuwa kamili, nje ya huyo hakuna mchezaji ambaye ana majeraha zaidi ya Rashid Juma ambaye aliumia kidogo kwenye mechi yetu ya mwisho kule Mara na Biashara United,” aliweka wazi Rweyemamu.

Comments are closed.