The House of Favourite Newspapers

Air Tanzania Inavyoipeleka Nchi Kwenye Uchumi wa Kati

Rais John Magufuli.

WAKATI Tanzania ikiwa katika harakati za kuingia katika uchumi wa kati, ni muhimu pia kwa wananchi kushiriki katika dhamira hiyo kwa kuvipa nguvu vyombo vya kitaifa au vya serikali kwa kushiriki katika kuboresha na kununua huduma zake.

 

Moja ya njia za kuimarisha uchumi wa nchi yetu ni kuliunga mkono shirika la ndege nchini, Air Tanzania Company Limited (ATCL) ambalo limepata nguvu mpya baada ya serikali ya awamu ya tano chini ya Rais John Magufuli kuliimarisha kwa kuleta ndege mbili aina ya Bombadier Q400NG ambazo zinafanya safari sehemu mbalimbali nchini.

Bombadier Q400NG.

Uhai mpya ulioletwa na serikali kwa shirika hilo ambalo ni mali ya wananchi, ulikwenda sambamba na kupangwa upya kwa watendaji na watumishi wake ikiwa ni pamoja na bodi mpya ya wakurugenzi na waziri mpya wa Ujenzi, Usafirishaji na Mawasiliano, Prof. Makame Mbarawa.

 

ATCL hivi sasa linatoa huduma katika miji mikuu ya mikoa mbalimbali nchini ikiwemo Songea, Bukoba, Dodoma, Kilimanjaro, Mtwara, Katavi, Mwanza na Dar es Salaam. Vilevile nauli za shirika hilo ni za kiwango cha chini kwa abiria wa kawaida na mizigo. Hivyo, moja ya njia za kuliimarisha ATCL ni kutumia huduma zake. Ukitumia ndege hizo za Bombadier, ATCL inafika pia katika nchi jirani zikiwemo za Burundi na Comoro. Nauli za ATCL siku zote zimekuwa ni nafuu zikilinganishwa na mashirika mengine ya ndege yanayotoa huduma hiyo nchini.

 

Kusafiri kwa kutumia vyombo hivi kutachangia kuongezeka na kukuza pato la taifa kuanzia kwa mtu mmoja, familia, mikoa husika na hadi taifa kwa jumla. Pamoja na kurahisisha mawasiliano baina ya watu kwa kuwepo kwa safari za ATCL sehemu mbalimbali nchini, shirika hilo pia linabeba jukumu kubwa la kusafirisha bidhaa mbalimbali ambazo ni muhimu kwa mahitaji ya wananchi, kibiashara, kijamii na katika hali mbalimbali kuwaunganisha wananchi kwa huduma nyingi zinazoweza kutolewa mkoa mmoja asubuhi na kufika katika mkoa mwingine baada tu ya saa chache au wakati mfupi.

 

ATCL lililoanzishwa mwaka 1977, ndiyo wapeperusha bendera wa Tanzania, makao makuu yake yakiwa jijini Dar es Salaam kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere. Lilianzishwa baada ya kutoweka kwa Shirika la East African Airways lililokuwa chini ya Jumuiya ya Afrika Mashariki awamu ya kwanza ambayo ilivunjika kutokana na kutoelwana kwa mambo kadhaa.

 

 

Shirika hilo lilikuwa linamilikiwa kikamilifu na serikali ya Tanzania hadi mwaka 2002 lilipobinafsishwa sehemu yake katika kuleta mabadiliko ya kiuchumi nchini kwa mujibu wa (taasisi za) Bretton Woods Institutions ambapo serikali ilipunguza hisa zake na kuwa asilimia 51 na ikaingia ushirika na shirika la South African Airways ambapo baada ya miaka minne na kuzinunua hisa zilizokuwa zimeuzwa na kulifanya kuwa shirika kamili la serikali.

STORI: MWANDISHI WETU

Comments are closed.