The House of Favourite Newspapers

AKIKUSALITI UKAMUACHA, WEWE NI MSHAMBA WA MAPENZI !

NI matumaini yangu kwamba una shauku kubwa ya kujua nini nimekuandalia kwa leo. Ni yaleyale kuhusu maisha yetu ya kimapenzi na leo nataka kuzungumzia usaliti katika sura ya tofauti.

Nimefikia uamuzi wa kuandika juu ya hili kutokana na ushuhuda nilioupata kutoka kwa mmoja wa wasomaji wangu aliyejitambulisha kwa jina la Fatma wa Tanga. Ni ushuhuda wa kusikitisha sana lakini una funzo ndani yake kwa wanandoa na wapenzi wa kawaida.

 

Anasemaje? Hebu msikie kwanza kisha tuendelee; “Mimi na mume wangu tulikuwa tunapendana sana na hajawahi kunisaliti. Tulioana miaka miatu iliyopita na sasa nina ujauzito wa miezi 7. “Mume wangu anafanya kazi na mimi pia nafanya kazi lakini kipato changu ni kikubwa kumzidi mume wangu.

 

“Kutokana na hali hiyo, mimi nilinunua gari ambalo mume wangu amekuwa akilitumia muda mwingi. Huwa ananipeleka kazini kisha yeye anaenda kwenye mihangaiko yake, jioni ananifuata. “Tunaishi na mdogo wangu wa kike ambaye anasoma chuo ila alionesha ukaribu sana kwa mume wangu, utani ulikuwa mwingi hadi kuna kipindi nikahisi kuna kitu kinaendelea kati yao kwa siri kubwa.

 

“Siku moja baada ya mume wangu kunipeleka kazini, tulimuacha nyumbani yule mdogo wangu, ilikuwa aende chuo lakini nikashangaa siku hiyo akasema hataenda. “Machale yakanicheza! Baada ya mume wangu kunifikisha kazini na kuondoka, nikakaa kama nusu saa hivi kisha nikachukua Bajaj na kurudi nyumbani.

 

“Huwezi kuamini nilimkuta mdogo wangu akifanya mapenzi na mume wangu juu ya kitanda changu. Nilipata presha na kuanguka, nimekuja kuzinduka niko hospitalini. “Mpaka sasa niko kwa wazazi wangu na nakaribia kujifungua. Hivi kwa usaliti huu nawezaje kumsamehe mume wangu na tukaishi kwa amani?”

 

Huo ni ushuhuda wa Fatma ambaye mwisho wa siku aliomba nimshauri. Ingekuwa wewe ungemshaurije? Je, ungemshauri arudi kwa mumewe au ungemtaka aombe talaka? Najua kwa vyovyote ungekuwa na la kumshauri lakini mimi ninavyoona kwa hili ni lazima uwe njia panda. Yaani mdogo wako umkute kamvulia nguo mumeo na wanafanya uzinzi juu ya kitanda chako! Ukisikia watu wanaua ni katika mazingira haya.

 

Related image

Hata hivyo kabla sijamshauri Fatma nikuulize wewe msomaji wangu, je, upo usaliti ambao unaweza kusema huu unavumilika na huu hauvumiliki? Kimsingi watu tunatofautiana jinsi tunavyopokea yale yanayotupata. Wapo watu ambao wamewafumania wanandoa wenzao mara kibao lakini mpaka leo bado wanaishi pamoja na wanasimamia ule msemo usemao; ‘Yaliyopita si ndwele, tugange yajayo’.

 

Lakini wakati hao wakiwa na mioyo hiyo, kuna ambao wameachana baada ya mmoja kukuta tu sms tata kwenye simu ya mwenza wake. Kwa hili la Fatma iko hivi, hakuna usaliti usiouma, uwe ni mdogo au mkubwa. Usaliti aliofanyiwa Fatma ni mkubwa sana, huwezi kumshauri kirahisi tu kwamba amsamehe mume wake na arudi kwake.

 

Lakini pia huwezi kumshauri kwamba kwa kuwa ni usaliti mkubwa basi asimsamehe na aombe talaka. Ushauri wote unaweza kuwa sawa lakini pia unaweza usiwe sawa. Kutokana na mazingira, kwamba Fatma ni mjamzito na mume wake hajawahi kumsaliti, kuna kila sababu ya kusamehe. Kama mume ameomba msamaha na kuahidi kubadilika, kumgomea itakuwa ni vigumu.

 

Lakini naomba niseme kwamba, kwenye suala la usaliti ni vyema tukazungumza na mioyo yetu. Ukijaribu kufuatilia utabaini hakuna ambaye hajawahi kusalitiwa na mpenzi wake. Tunachokifanya huwa ni kusamehe na kusahau hasa tukichukulia kwamba, wote tuna mapungufu. Ni kweli kuna usaliti usiovumilika, kwa mfano kama amekuwa akikusaliti kila wakati, huyo ifike wakati useme imetosha.

 

Lakini kama unampenda na kwa bahati mbaya akawa amekusaliti kwa mara ya kwanza, ni vyema ukampa nafasi nyingine bila kujali watu watasemaje. Kwa maana hiyo licha ya kwamba usaliti si mzuri lakini usichukue uamuzi wa kumuacha mwenza wako au mpenzi wako kwa sababu ya usaliti wa mara ya kwanza, ukifanya hivyo kuna watakaokuona ni mshamba wa mapenzi na ipo siku utajuta.

Ni hayo tu kwa leo, tukutane tena wiki ijayo kwa makala nyingine.

Comments are closed.