Akili ni Kiwanda na Wazo Malighafi
AKILI hufafanuliwa kuwa ni uwezo wa kufikiri na kufanya maamuzi; maamuzi yanaweza kuwa ya busara au si ya busara. Akili, pia ni uwezo wa kuelewa mambo, kufahamu na kutafakari.
Kuwa na akili ina maana mtu ana uwezo wa kuamua mambo kwa kutumia akili. Ni wazi kwamba kutumia akili ni kutumia uwezo wa kufikiri. Hata hivyo, watu wengi huacha wengine wafikiri kwa niaba yao badala ya kujiamulia mambo wenyewe. Watu hao hutumia maoni ya wengine kutoka katika vyombo vya habari na sehemu mbalimbali ambako maarifa hupatikana.
Wazo ni zao la fikra, na ili mtu apate wazo ni lazima afikirie. Wazo ni ujumbe unaotumwa kutoka akilini kwa viumbe hai vyenye ufahamu ili kujua kutenda jambo bila kukosea. Wakati wa kufikiria jambo ndipo akili hutumika, hivyo basi akili na wazo huathiriana na hutegemeana.
Fikra husaidia maamuzi kwa vile mwanadamu ni tofauti na viumbe vingine kwa utashi wa fikra, tofauti na wanyama ambao mara nyingi huishi bila ya kufikiri, yaani kujua nini atafanya kesho au ataishi vipi. Lakini mwanadamu hutumia fikra na kuvumbua vitu ambavyo vinahitajika.
Akili ni kiwanda na wazo ni malighafi ambayo baadaye inakuwa bidhaa. Akili ni kiwanda kwa kuwa kiwanda huboresha malighafi kuwa bidhaa. Wazo linazalishwa na akili na baadaye wazo hilohilo linaboreshwa kuwa kitu kingine ambacho ni bidhaa.
Katika mawasiliano ya data wazo (ideas) imekuwa ni kitu muhimu sana kwani ndiyo malighali ambayo akili huiboresha na kuwa bidhaa. Ushindani wa soko, elimu, sayansi na teknolojia hutegemea sana vitu hivi viwili akili na wazo.
Bila fikra duniani tusingeweza kuishi pamoja kwa kusaidiana, tungekuwa sawa na wanyama, hivyo dunia isingekuwa sehemu nzuri ya kuishi.
Salum Milongo/GPL
Comments are closed.