The House of Favourite Newspapers

Albino atoweka kimaajabu Mkuranga

0

A.Kaimu Katibu Mkuu wa Chama Cha watu wenye Ulemavu wa Ngozi (Albino),Josephat Torner akizungumza na wanahabari juu ya uakatili dhidi yao. Kaimu Katibu Mkuu wa Chama cha Albino Tanzania, Josephat Torner (watatu kutoka kulia) akizungumza na wanahabari juu ya ukatili dhidi yao.
B.Shemeji wa Said aliyepotea aitwae, Waziri Bakari akionesha hisia zake kwa wanahabari (hawapo pichani).Shemeji wa Said Abdallah (watatu kutoka kulia), Waziri Bakari akionesha hisia zake kwa wanahabari (hawapo pichani).
C.Mkutano ukiendelea na wanahabari.Mkutano ukiendelea na wanahabari.

Dar es Salaam, Tanzania

HUZUNI! Mtu mmoja anayedaiwa kuwa na ulemavu wa ngozi (Albino), Said Abdallah (47), anadaiwa kupotea katika mazingira ya kutatanisha katika Kijiji cha Mbezi Mlungwana wilayani Mkuranga, Pwani.

Akizungumza na wanahabari leo jijini Dar es Salaam, Kaimu Katibu Mkuu wa Chama cha Albino Tanzania, Josephat Torner, amesema kuwa chama chao kwa kushirikiana na Shirika la Under The Same Sun, wanatangaza kupotelewa na mwenzao huyo aliyepotea Januari 31, mwaka huu wilayani humo.

Torner amesema mara ya mwisho kabla hajatoweka, Abdallah aliwaaga wenzake anaoishi nao kuwa anakwenda kuuza mboga za majani katika Kijiji cha Mtipule ambacho kipo kati ya Kijiji cha Nyakenge na Kitongoji cha Kaloleni ambapo ameeleza kuwa siku hiyo alionekana katika kilabu inayouza pombe za kienyeji huko Mkuranga.

Kwa mujibu wa taarifa za wakazi wa Mtupile zilieleza kuwa, siku hiyo ya Janauri 31, Abdallah aligombana na wenzake aliokuwa akinywa nao pombe majira ya saa moja na nusu usiku na kisha aliondoka kilabuni hapo na kuelekea kusikojulikana.

Alifafanua kuwa kwa mujibu wa ndugu zake walipoona ndugu yao hajarudi tangu aondoke, waliamua kwenda Kituo cha Polisi cha Kimanzichana, Mkuranga na kupewa RB namba KIM/RB/502016 na kama hiyo haitoshi pia waliamua kupeleka taarifa katika kituo kikuu cha Mkuranga na kupewa RB namba MKU/PE/05/2016, huku wakiomba kwa yeyote atakayemuona atoe taarifa katika kituo cha polisi kilichopo karibu nae.

Kutokana na kutoweka kwa Abdallah, Torner amefafanua kuwa  chama chao kwa kushirikiana na Shirika la Under The Same Sun, wanasikitishwa na kushamiri kwa matukio ya aina hii ikiwa ni pamoja na tukio la kutekwa nyara mtoto mdogo wa kiume mwenye albino, Tito Nkuryu (3) huko Itilima Mkoa wa Simiyu usiku wa kuamkia Februari ambapo baada ya kumwokoa alipelekwa kituo cha kulelea watoto, Lamadi.

Aliongeza kuwa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na lile la Afrika Mashariki, kwa pamoja yanapaswa kujadili kwa kina juu ya mauaji dhidi ya watu wenye ulemavu wa ngozi (albino) kuweza kupatikana ufumbuzi kamili dhidi yao ili waweze kuishi kwa amani hapa nchini.

Na Denis Mtima/GPL

Leave A Reply