Alichokifanya Nyerere baada ya Uhuru
Tunaendelea kuelezea habari ya Mwanasiasa Zuberi Mtemvu aliyepingana na Mwalimu Nyerere kabla ya uhuru:
Kilichofuata baada ya kupatikana uhuru mwaka 1961 ilikuwa ni kukamatwa, kuwekwa kizuizini na kuhamishwa kwa baadhi ya wapinzani waliodhaniwa kuwa wanapinga utawala wa Mwalimu Nyerere.
Miongoni mwa waliokamatwa ni Abdillah Schneider Plantan, Sheikh Abdulkarim Abdulwahid, Maalim Popo Saleh, Suleiman Masudi Mnonji, Ali Migeyo, Mufti Sheikh Hassan bin Amir, Sharff Hussein Badawiy, Shariff Mwinyibaba na Shariff Adnan.
Wengine ni Bilali Rehani Waikela, Sheikh Jumanne Bias, Maalim Matar, Abdallah Mwamba, Sheikh Hashim Haji Abdallah, Sheikh Nurdin Hussein, Salum Abdallah Popo, Sheikh Mzee Ali Comoriam, Sheikh Al Amin Maftah, Rajab Kiguu cha Mbuzi na wengine wengi.
Lakini ukweli ulikuwa kwamba si wote katika wale waliokamatwa na kuwekwa kizuizini walijihusisha na siasa. Baadhi yao walikamatwa kwa sababu tu walikuwa wakishirikiana na wale waliodhaniwa ni wapinzani wa Mwalimu Nyerere.
Maalim Matar na Shariff Adnan walifungwa jela kwa sababu tu walihusika na Msikiti wa Badawiy mjini Dar es Salaam ambako Sheikh Hassan bin Amir, wakati huo akichukuliwa kuwa ndiyo roho ya waumini wa Tanganyika, alikuwa akiendesha madrasa yake kila magharibi pale msikitini, kilichofanywa wakamatwe ni siri ya wana usalama.
Shariff Hussein na nduguye Mwinyibaba walihamishiwa Kenya, walikotoka si kwa sababu ya Uislamu wao bali Nyerere alielezwa kwamba walikuwa wamejishughulisha katika harakati za kuipinga serikali yake.
Sheikh Mzee Ali Comorian alitiwa kizuizini kwa sababu kila mara alikuwa akifuatana na Sheikh Hassan bin Amir kama vile alikuwa kivuli cha sheikh. Kilichomfanya Nyerere kuwatia kizuizini watu hao na wengine kuhamishwa ni kile kilichoelezwa kuwa ni usalama wa taifa lakini Zuberi Mtemvu alisalimika.
Itaendelea wiki ijayo.