The House of Favourite Newspapers

Aliyetajwa na JPM Kukamatwa na Mabilioni Airport, Afikishwa Mahakamani

Mshtakiwa akifikishwa kortini.

IKIWA ni takribani siku 9 baada ya Rais Dkt. John Magufuli kubainisha kukamatwa kwa mtu aliyekuwa akiingiza nchini kiasi kikubwa cha fedha za kigeni katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), dar es Salaam, mtuhumiwa aliyekamatwa na fedha hizo amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kujibu tuhuma zinazomkabili.

 

Businge Winfred (33), Raia wa Uganda ambaye ni Kalani wa Kampuni ya Ulinzi ya SGA, aliyekamatwa Desemba 11, 2017 uwanjani hapo na kiasi cha Dola Milioni 1 (Tsh Bilioni 2.2), amesomewa mashtaka ya kushindwa kuzitolea maelezo fedha hizo kwa mamlaka ya forodha.

 

Wakili wa serikali Mwandamizi, Awamu Mbagwa ameieleza mahakama mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi kuwa mshtakiwa anakabiliwa na kosa moja ambalo amelitenda kinyume na kanuni za sheria za utakatishaji fedha huku akieleza kuwa kosa hilo halimnyimi mshtakiwa kupewa dhamana.

 

Mshtakiwa amekana kosa hilo, ambapo wakili Mbagwa ameieleza mahakama kuwa upelelezi wa kesi hiyo umekamilika na ameomba tarehe kwa ajili ya kumsomea mshtakiwa maelezo ya awali.

Baada ya maelezo hayo, wakili wa upande wa utetezi Emmanuel Safari alimuombea dhamana mteja wake ambapo Hakimu Shaidi aliruhusu mshtakiwa huyo kuachiwa kwa masharti ya dhamana ya mdhamini mmoja bila kusaini bondi kwa sababu fedha zilizokamatwa zitakuwa kama dhamana yake. Kesi imeahirishwa hadi January 18,2018.

Mabilioni Yakamatwa Airport Yakiingizwa Tanzania

Comments are closed.