Na Issa Liponda: Rais wa chama cha Soka la Wanawake Tanzania, Amina Karuma amesema kuwa umefika wakati wa wachezaji wa soka la Wanawake nchini kupata nafasi ya kucheza soka la kulipwa.
Karuma aliyasema hayo jana Ijumaa alipofanya ziara katika ofisi za Global Group zilizopo Sinza Mori jijini Dar es salaam na kujionea shughuli mbalimbali zinazofanywa na kampuni hiyo inayozalisha magazeti Pendwa, magazeti ya michezo ya Championi na Spoti Xtra, +255 Global Radio na Global TV Online.
Akizungumzia nafasi ya soka la Wanawake nchini Karuma alisema: “Tulipotoka na hapa tulipofika kiukweli tunaona mwanga katika soka la Wanawake, timu zetu za Taifa zimekuwa zikifanya vizuri katika mashindano mbalimbali.
“Licha ya kuwa hatukufanya vizuri katika Mashindano ya Afrika Mashariki na kati (Cecafa) yaliyofanyika hapa nchini lakini bado sisi ni bora sana.
“Upande wa ligi tupo vizuri sana na ndiyo maana ligi yetu ni miongoni mwa ligi tatu bora barani Afrika, dhumuni letu sasa, tunataka mpira wa Wanawake uhame kutoka kuwa wa ridhaa hadi kuwa soka la kulipwa yaani wachezaji wetu wawe profesheno.
“Tukifanikiwa katika hilo ndipo tutakapotafuta njia kwa wachezaji wetu waende nje wakacheza soka la kulipwa,” alisema Karuma.
Aidha Karuma aligusia pia juu ya maandalizi ya timu ya Taifa ya U17 ambayo itacheza mchezo wa kufuzu Afcon januari 12 dhidi ya Burundi hapa, ambapo alisema timu ipo kambini na inaendelea na maandalizi ya mchezo huo.
Karuma alipokelewa na kiongozi wa 255global radio, Borry Mbaraka sambamba na kiongozi wa Global TV Online, Kelvin Nyorobi, ambapo kwa pamoja walimtembeza maeneo mbalimbali.
Pia, alipata nafasi ya kukutana na Mhariri Mtendaji wa Global Publishers, Saleh Ally ‘Jembe’ na kuzungumza naye masuala kadhaa yahusuyo soka la Wanawake.
Pia alimpongeza Saleh kwa kitendo cha kutoa zawadi ya njumu pea mbili kwa mchezaji wa Yanga Princess, Fatuma Bushiri.