The House of Favourite Newspapers

AMINI : LINAH KATULIA KWANGU , TENA AMENASA

UKISIKIA majina ya wasanii Amini Mwinyimkuu na Asterlina Sanga ‘Linah’ bila shaka kichwani kibao kitakachogonga kwenye kumbukumbu zako ni ‘Mtima Wangu’ cha Amini akishirikiana na Linah.

 

Hawa ni wanamuziki wakali wanaotesa kwenye muziki wa Bongo Fleva. Sauti zao ni hatari, kolabo yao inafiti vilivyo na kuwafanya mashabiki wapagawe pindi wanapovamia jukwaa pamoja. Ni enzi zile wakati kapo yao ikitamba wakiwa katika Jumba la Vipaji Tanzania – Tanzania House of Talent (THT). Wawili hao walidumu kwa muda mrefu, kisha baadaye wakamwagana.

 

Amini alioa na Linah aliolewa na mwanaume mwingine. Lakini wote kwa sasa wamemwagana na wenzi wao na inaelezwa kuwa wamerudiana. Awali yalikuwepo madai kuwa penzi lao limefufuka lakini kuna waliokuja baadaye na kusema kuwa hapakuwa na chochote zaidi ya kuwa wanatafuta kiki tu.

 

Magazeti yetu ya Global Publishers, yamewahi kufanya mahojiano na Amini ambaye alikiri kurudiana na Linah na kusema kuwa, imetokea hivyo kwa sababu yeye alikuwa singo baada ya kuachana na mkewe na Linah naye alikuwa katemana na baba wa mtoto wake aitwaye Shebby.

 

Kwa maelezo hayo ilikuwa rahisi watu kuamini kuwa penzi lao limerejea lakini Linah hapo kati aliibuka na kukanusha kurudiana na Amini.

Licha ya kukanusha huko, bado wawili hao waliendelea kuwa pamoja, mapichapicha yao ya kimalovee yakawa yanatrendi sana huko kwenye mitandao ya kijamii, hapo ndipo wadau walipohitimisha kuwa wamerudiana ila Linah hataki tu kufunguka ukweli.

 

Pamoja na kuwa kwao karibu kuelezwa kuwa ni kutokana na kufanya muziki pamoja huku wakiendelea kupeana penzi kwa siri, juzikati polisi wa Risasi Jumamosi alimtafuta tena Amini na kufanya naye mahojiano ambapo alifunguka baadhi ya mambo ikiwa ni pamoja na kilicho nyuma ya pazia kuhusu yeye na Linah.

 

Fuatilia mahojiano hayo:

MIKITO: Kuna kipindi hapo nyuma kidogo ulipotea kwenye ulimwengu wa muziki, mashabiki wako wakaanza kukusahau kimtindo, nini kilichokuwa kimesababisha hali hiyo?

AMINI: Kupotea kwangu siyo kwamba nilikuwa siingii studio bali kuna kazi za kijamii nilikuwa nafanya kama za kwenda vijijini, hivyo ilikuwa ngumu nitoe nyimbo mimi sipo, niagize tu mtu anisimamie. Ndiyo maana kidogo nilikuwa kimya.

MIKITO: Sasa hiyo kukaa kimya huoni kama ilikupotezea mashabiki?

AMINI: Unajua mtu mwingine anaweza kufikiri hivyo lakini ukweli ni kwamba, msanii wa kweli atabaki tu, hata asipoimba kwa muda gani mashabiki wake wataendelea kuwa naye, atapotea lakini akirudi wataendelea kuwa naye na kumpa sapoti kama kawaida.

MIKITO: Tunachojua ni kwamba umekuwa ukitegemea sana muziki kuyaendesha maisha yako, sasa wakati ulipokuwa umekaa kimya kwenye game la muziki, ulikuwa ukipata pesa kwa njia gani?

AMINI: Kazi za kijamii nilizokuwa nafanya wakati huo ndizo ambazo zilikuwa zikinipatia pesa ambazo zilinisaidia kujikimu kimaisha.

MIKITO: Ulikuwa kwenye ndoa lakini kuna madai kwamba, Linah ndiye aliyesababisha ukaachana na mkeo, kuna ukweli wowote katika hilo?

AMINI: Hapana! Unajua watu wanaongea sana bila kujua ukweli, wanavyofikiria ni tofauti kabisa.

MIKITO: Sasa ni kipi hasa kilichosababisha wewe na mkeo muachane?

AMINI: Unajua hayo ni mambo binafsi ambayo siwezi kuyaweka hadharani. Nafanya hivi kwa sababu kuna mtu ikiandikwa hiyo habari atakata kipande cha gazeti akabandike kwake, siku mtoto wangu akikua na kusoma itakuwa sio jambo zuri kabisa.

MIKITO: Kwa maana hiyo umeamua kurudisha majeshi kwa Linah, si ndiyo maana yake?

AMINI: Tulipoachana mimi na Linah, ilikuwa kiroho safi, hakuna aliyegombana na mwenzake. Kingine ni kwamba, si unajua true love never die? (penzi la kweli halifi?). Kwa hiyo ndiyo hivyo amerudi kwangu na amenasa.

MIKITO: Hivi mlibahatika kupata mtoto wewe na yule mkeo?

AMINI: Ndio, Mungu alitujaalia mtoto tena dume la mbegu.

MIKITO: Basi nashukuru sana na nakutakia kila la heri katika shughuli zako za kila siku.

AMINI: Asante sana!

Comments are closed.