Amuua Mkewe, Amchoma Kwa Mkaa Gunia 2 na Kuwa Majivu
JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, linamshikilia mwanamme mmoja kwa jina la Khamis Luwoga maarufu kama ‘Meshack’ kwa tuhuma za kumuua na kumchoma moto mke wake Naomi Marijani (36). Mwanamke huyo anadaiwa kutoweka katika mazingira ya kutatanisha na picha yake kusambazwa katika mitandao ya kijamii sanjari na taarifa za kutoweka kwake.
Mkuu wa Upelelezi kanda hiyo, Camillius Wambura, alisema wanamshikilia mtuhumiwa kwa mahojiano na kwamba polisi walikwenda kwenye maeneo ambayo mtuhumiwa aliyataja kufanyia mauaji na wamechukua majivu kwa ajili ya vipimo vya DNA ili kupata uthibitisho. Kwa mujibu wa taarifa hizo, inadaiwa kuwa Luwoga na mke wake Naomi hawakuwa na maelewano ya muda mrefu.
Kwa mujibu wa taarifa ya Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Kigamboni, Thobias Walelo, mtuhumiwa huyo amekiri kumuua mkewe na kisha kumchoma kwa mkaa magunia mawili na kumzika shambani kwake ambapo katika maelezo yake amedai mara baada ya mauaji hayo aliuchukua mwili na kuuweka kwenye shimo alilochimba kwenye banda lake la kufugia kuku.
Amedai baada ya kuuweka shimoni aliweka mkaa magunia mawili na mafuta ya taa kisha akawasha moto ulioteketeza mwili wote hadi kubaki majivu kisha alichukua majivu hayo akaweka kwenye mfuko na kubeba kwa kutumia gari lake lenye namba T206 CEJ, Subaru Forester yenye rangi nyeusi na kuupeleka shambani kwake lililoko Kijiji cha Mlogolo, mkoani Pwani.
“Alichimba shimo kwenye shamba lake kisha kuweka hayo majivu, akayafukia na akapanda mgomba juu yake, kisha akaanza kusema mke wake ametoroka nyumbani Mei 15 na kufungua taarifa polisi ambako alipewa RB ya kituo kidogo cha Mjimwema MJ/RB/234/2019.
Naomi alitoweka nyumbani kwake Mei 15, 2019, ambapo familia yake ilitoa taarifa za kutoweka kwake katika kituo cha Polisi Chang’ombe, baada ya Luwoga kuwapa taarifa siku nne baada ya Naomi kutoonekana nyumbani.
Comments are closed.