Arteta Afunguka Ishu ya Martinelli
BOSI wa Arsenal, Mikel Arteta ametaja sababu ambazo zinamfanya kinda wa timu hiyo, kushindwa kuanza kwenye kikosi cha kwanza.
Arteta amesema kinda huyo amekuwa akishindwa kuanza ndani ya kikosi hicho kutokana na kukosekana muunganiko kati yake na wachezaji wenzake kwa siku za hivi karibuni.
Martinelli amekuwa na hali hiyo baada ya kupata majeraha ambayo yalimfanya awe nje tangu Juni, mwaka jana akisumbuliwa na goti.
Straika huyo baada ya kuwa nje kwa muda mrefu, alirejea uwanjani Desemba, mwaka jana lakini akaumia tena enka kwenye Kombe la FA walipocheza dhidi ya Newcastle.
“Alirejea uwanjani kutoka kwenye majeraha, ila akapata tena kwa hiyo hivi sasa kinachofanyika ni kutengeneza muunganiko kati yake ya wenzake ndiyo maana unakuta haanzi.
“Mnaweza kuwa mmesahau, kuna wakati tulicheza dhidi ya Man United na yeye alianza na wachezaji wengine wakasubiri. Najua wote mnafahamu uwezo wake, ataimarika na kuwa bora zaidi.
“Pia kwa sasa kuna vitu vingi anatakiwa kujifunza na kuvifanyia kazi, lakini kwa umri bado na pia yupo kwenye ligi ambayo sio rahisi na mbaya akapata majeraha,” alisema Arteta.