The House of Favourite Newspapers

Asha Baraka: Karate ilimpa umaarufu Tabora Girls

Mwandishi: Boniphace Ngumije | CHAMPIONI| STAA ANAYEFUNGUKA

MPENZI msomaji wa kolamu hii inayohusu maisha ya mastaa, karibu katika safari nyingine ya simulizi ya kuvutia, kuburudisha, kusisimua na kufundisha kutoka kwa mwanamama mwenye jina kubwa katika Tasnia ya Muziki wa Dansi, Bongo, Asha Baraka ambaye pia ni Mkurugenzi wa Bendi ya The African Stars ‘Twanga Pepeta’.

Asha Baraka ndiye mwanamama pekee Bongo anayemiliki bendi ikiwa inaundwa na timu ya wanaume pamoja na wanawake. Ana mengi sana ya kukusimulia hapa, ili kufahamu ametokea wapi, amepitia changamoto zipi mpaka mafanikio, ilikuwaje akajiingiza kwenye masuala ya kudhamini bendi, maisha yake binafsi pamoja na mengine mengi?

Fuatilia kuanzia mwanzo mpaka mwisho wa simulizi hii. Songa nayo… ASHA Baraka anaanza kusimulia kuwa, amezaliwa katika Kijiji cha Kibingo Kata ya Mwandiga mkoani Kigoma.

Ni mtoto wa sita kati ya watoto tisa katika tumbo la mama yake, lakini jumla ya watoto waliozaliwa kwa baba yake ni 21, maana alikuwa na wake wawili. Kwenye tumbo lao wakiwa tisa, huku mama yao mwingine akiwa na watoto 12. Asha Baraka anaendelea kuwa amezaliwa katika familia yenye maisha ya kati kiuchumi, japo baba yake alikuwa ni

Mwanamuziki Asha Baraka

Mganga Mkuu katika Hospitali ya Kibingo lakini mshahara aliokuwa anaupata ulikuwa hautoshi kutokana na kuwa na familia kubwa. Akisimulia kuhusu maisha yake ya utotoni, Asha Baraka anasema kuwa alikuwa ni mtoto mtundu sana.

Akiwa tu Shule ya Msingi Kipaupa, mara kwa mara alikuwa anajikuta katika ugomvi na baba yake mzazi kwa sababu alikuwa hapendi kuvaa mavazi ya kike pamoja na michezo aliyokuwa anapendelea. “Kiukweli nilikuwa sipendi kabisa kuvaa sketi wala mavazi mengine kama watoto wa kike wengine.

Nilipendelea zaidi kuvaa suruali na hata michezo yangu ilikuwa ni kama ya watoto wa kiume, nilipenda kupanda miti, kukimbia riadha na kucheza mpira wa pete. “Sasa kuhusu hayo yalikuwa hayapendezi k w e baba yangu, alihitaji niwekama watoto wa kike wengine lakini mimi haikuwa hulka yangu kabisa,” anasimulia Asha Baraka. Anaendelea kuwa katika maisha yake hayo ya utotoni, kutokana na utundu amepitia matukio mengi mno, moja ambalo hawezi kulisahau ni pale alipokuwa darasa la saba, baada ya kuhama shule kutoka Kipaupa kwend a Shule ya Msingi Nguruka baada ya baba  yake kuhamishwa kikazi.

Anasema ikiwa ni wiki moja tu kabla ya kufanya mtihani wa kumaliza darasa la saba, kama kawaida yake alikwenda kupanda miti na watoto wenzake, akiwa huko alidondoka kutoka juu mpaka chini na kuvunja mkono, kwa hiyo akalazimika kufanya mtihani akiwa na P.O.P. Hata hivyo anaendelea kusimulia kuwa Mungu alimsaidia akafaulu mitihani yake ya darasa la saba na kuchaguliwa katika Shule ya Sekondari ya Wanawake Tabora (Tabora Girls).

“Huko maisha pia yaliendelea kama kawaida, lakini tabia zangu za kiume sikuweza kuziacha badala yake zikawa zinazidi kukua, nikaendelea pia kupenda michezo hasa mpira wa pete, riadha na wakati huu nikaanza kujifunza michezo ya karate ili kujilinda.

“Unajua kipindi hicho kulikuwa na makundi ya vijana watukutu yaliyoibuka, watu waliosoma Tabora miaka ya nyuma watakumbuka juu ya makundi haya ya vijana waliokuwa wanajiita Break Septemba (panya road ya sasa), vijana hawa w a l i k u w a hatari sana na walikuwa wanavizia wanafunzi njiani na kuwapora pamoja na ku

watendea masuala mengine ya udhalilishaji,” anasema Asha Baraka. Anaendelea kuwa baada ya kuiva kwenye karate akageuka kuwa mtetezi wa wanafunzi wenzake hasa pale walipovamiwa na vijana hao wa Break Septemba, anasema jambo hilo lilimpa umaarufu sana shuleni kwao na hata vijana wakaanza kumuogopa hasa wale waliokuwa wanammezea mate kimapenzi!

Asha Baraka anazidi kusimulia kuwa pamoja na umaarufu huo wa kufahamu karate, kupewa uongozi shuleni ili tu kumuepusha na maisha ya utundu aliyokuwa anaishi, pia kwenye mpira wa pete, nako mambo yaliendelea kuwa mazuri ambapo ikafikia hatua mpaka akachaguliwa kwenye timu ya Mkoa wa Tabora.

“Hayo yote hayakutosha kunifanya mimi kujiona fahari shuleni, ni kweli nilikuwa maarufu lakini nilifahamu kuwa nilitakiwa kuwa na pesa ili kuifanya heshima yangu kukuwa zaidi kutokana na kuwa shuleni kuna baadhi ya wasichana waliotokea kwenye familia bora, waliringa kwa pesa za wazazi wao.

“Kutokana na hilo ikabidi nianze masuala ya ujasiriamali nikiwa shuleni, yaliyonipatia pesa sana!” Je, ni ujasiriamali wa nini Asha Baraka alianza kufanya? Vipi kuhusu maisha yake ya uhusiano wa mapenzi? Vipi kuhusu mavazi ya kiume, ataacha kuvaa? Usikose kufuatilia Jumatatu ijayo.

Comments are closed.