The House of Favourite Newspapers

Askari JWTZ Atiwa Mbaroni kwa Tuhuma za Kutengeneza Vyeti Feki

0
vyetiPOLISI mkoani Kigoma imewatia mbaroni watu watano akiwemo askari mmoja wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kwa tuhuma za kutengeneza vyeti bandia vya kitaaluma, miongoni mwake vikiwemo 90 vya uuguzi, ambavyo vilikutwa vikisubiri kugawiwa kwa wahusika.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kigoma, Ferdinand Mtui alisema kuwa pamoja na vyeti hivyo vya uuguzi vilivyokamatwa, pia katika operesheni hiyo walikamata vyeti 37 vya wataalamu wa maabara na vyeti tisa vya ufamasia.
Alisema kuwa katika operesheni hiyo iliyofanywa kwa pamoja na maofisa kutoka Baraza la Wafamasia nchini, walikamata jumla ya vyeti 936 vikiwa kwenye hatua ya ukamilishaji vikiwa bado havijaandikwa majina, miongoni mwake vikiwemo vyeti 667 vya wauguzi wasaidizi, vyeti 126 vya wataalam wa maabara, cheti kimoja cha mafunzo ya afya ya jamii na vyeti viwili vya utoaji huduma ya kwanza.
Katika kuhakikisha wanakuwa na uthibitisho wa tuhuma hizo, Kamanda Mtui alisema kuwa pia wamekamata mihuri 25 ya taasisi mbalimbali ikiwemo nyundo mbili, ambazo hutumika kutengenezea mihuri mbalimbali ya moto.
Aliwataja watu waliokamatwa katika operesheni hiyo ambayo inahusisha mtandao wa watu mbalimbali kuwa ni askari wa JWTZ, Mgeni Nyamubozi ambaye ni mume wa mmiliki wa Duka la Vifaa vya Ofisi la Upendo, lililopo Mwanga mjini Kigoma, ambalo linatuhumiwa kuhusika na utengenezaji wa vyeti hivyo.
Katika duka hilo, Kamanda huyo wa polisi alisema polisi walikamata kompyuta mpakato moja, ikiwa na nakala za vyeti mbalimbali za vyuo na idara za serikali.
Mwingine aliyekamatwa ni Dickson Mshahili, muuguzi katika Hospitali ya Mkoa Kigoma ambaye katika upekuzi nyumbani kwake, alikutwa na nyaraka mbalimbali ikiwemo madaftari 12 yakiwa na kumbukumbu za vyeti anavyotengeneza na mihuri ya waganga wakuu wa mikoa ya Kigoma, Kagera, Mwanza, Singida na Tabora.
Sambamba nao alikamatwa Zawadi James, muuguzi wa Kituo cha Afya Ujiji ambaye baada ya kupekuliwa nyumbani kwake, alikutwa na vyeti vitatu na kabuleta ya pikipiki ambayo hutumika kutengeneza mihuri ya moto.
Wengine waliokamatwa ni Johnson Nyabuzoka, mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Mlole ya mjini Kigoma, ambaye ni mtaalam wa kompyuta aliyekuwa akitumika kufanya kazi hiyo; na Stephano Erasto ambaye alikamatwa katika siku yake ya kwanza tangu ajiunge na duka hilo kwa ajili ya kusaidia kazi.
Mihuri iliyokamatwa katika tukio hilo.
Kompyuta mpakato,Laptop,Printer na Scarner pamoja na mihuli  ni vifaa vilivyokamatwa katika Steshanari hiyo
Leave A Reply